Header Ads Widget

Responsive Advertisement

SIMULIZI FUPI - DAWA YAKE NDOGO SANA


Zainab ni binti mrembo lakini jeuri sana. Tangu utoto wake amekua mkaidi na jeuri. Mama yake hakuwa mkali sana japo baba yake alikua akimpiga na kumgombeza mara kwa mara. Zainab alikua akitaka chochote ni lazima apate, angeomba na kama angenyimwa basi angesusa kula mpaka akipate anachotaka. Mama yake aliumizwa na tabia zake kwani hakupenda jinsi alivyokua jeuri
Shuleni pia Zainab alipigwa na walimu mara kadhaa. Alichelewa kufika shule, alipiga kelele darasani,alikua mtukutu na mchokozi kwa wenzake. Alikua na marafiki wengi kwani kuna ambao walijipendekeza kwa kumuogopa kwajili ya ubabe wake. Hata ambao hawakumpenda hawakuwa na cha kumfanya kwani alikua mkorofi, mbabe na mjanja sana kiasi kwamba hata watoto wa kiume hawakumuweza
Kuna siku aligombana na kijana wa kiume aliyemzidi umri na nguvu. Alipoona hana cha kumfanya, alimvizia wakati wa kutoka na kumsukumiza kwenye shimo lililokuwa limechimbwa kwajili ya taka za shule. Kuna wakati alitumia mawe au kitu chochote kuwapiga watu walomzidi nguvu.
Baada ya kumaliza shule ya Sekondari Zainab alikaa miaka kadhaa na kisha kuolewa na mwanaume mmoja aliyempenda sana lakini alimzidi miaka kama nane hivi. Mwanaume huyu japo alimpenda mke wake lakini alikua mkali pia. Yeye hakuwa na mkono wa kupiga, lakini alimpa adhabu mke wake kila alipoleta ujeuri. Kuna wakati alimpa adhabu za kumfungia ndani, kumnyima pesa ya matumizi au kutomuongelesha kwa hata wiki nzima, lakini adhabu hizo zote zilikuwa kama zisizo na maana kwa mkewe. Mwanamke huyu aliendelea kuwa jeuri, mwenye kiburi na mkorofi hata kwa mumewe
Siku moja bi. Zainab na ukorofi wake alikasirika na kuchana nguo kadhaa za mumewe. Mumewe kwa kumkomesha akamwambia kuna taarifa amepokea na hivyo anatakiwa kusafiri kwenda kijijini kwao mara moja. Hakujali kuwa mkewe kaelewa au la na pia hakumwambia hasa ni nini kinampeleka. Alichofanya ni kuondoka tu. Kwakuwa walikuwa katika ugomvi, Zainab alijidai kutojali sana kuhusu safari ya ghafula ya mumewe na kumuacha tu aende.
Jamaa alimuacha mkewe jeuri na kusafiri na alipofika huko alizima simu. Kwa muda wa wiki ya kwanza Zainab alijifanya hajali kuhusu mawasiliano
Wiki ya pili alijaribu kumtafuta bila mafanikio
Wiki ya tatu alianza kupagawa na kukosa amani
Wiki ya nne aliwataarifu wazazi wake ambao walikua wanajua ukorofi wake hivyo walijua anaadhibiwa tu, kwani mumewe alikua amewapigia na kuwambia mpango wake

Zainab alianza kupunguza kilo moja baada ya nyingine kwani tangu mwanzo wa ndoa yao mumewe hakuwahi kulala nje ya nyumbani wala hata kusafiri kwa zaidi ya wiki moja bila yeye, lakini na pia alimuonesha kumpenda sana kiasi kwamba haingekuwa rahisi kukaa siku zote hizo bila mawasiliano
Zainab alipata tabu ndani ya mwezi mzima huku akiwa hana msaada. Aliwaza mara kadhaa alizomfanyia mumewe ukorofi na kuwa mkaidi na alijiona kwa ujinga na upumbavu wake anamfanya mumewe amkimbie. Kwa mara ya kwanza alianza kujutia tabia yake mbovu.
Alikaa na kuandika makala ndefu kwa mumewe akiomba msamaha na kutubu kwa tabia zake. Aliahidi hangerudia tena na alijiorodheshea makosa yake yote huku akiahidi kuyaacha. Kesho yake alienda kuongea na mama yake na kujieleza jinsi gani anajutia ujeuri wake unavyomfanya ampoteze mume, na kumwambia mama yake kuwa kwa sasa ameamua kabisa kubadilika. Mama yake hakuamini kwani mara kadhaa Zainab alionywa lakini hakuonekana kama mtu mwenye mpango wa kubadilika.
Baada ya siku kadhaa mumewe alirudi. Alipompa aisome barua ndefu aliyoandika, hakuamini kama kweli hiyo ndiyo ilikuwa tiba ya ndoa yao, lakini kuanzia siku hiyo Zainab alikuwa mtu mpya mwenye heshima, adabu na mapenzi ya kweli kwa mumewe.

Post a Comment

0 Comments