Header Ads Widget

Responsive Advertisement

LOVE BITE - 5




Simulizi : Love Bite
Sehemu Ya Tano (5)

“OOOOH MY GOD……..WHY ME?????”

Alijikuta nguvu zinamuishia Jothan na kukaa chini. Aliiangalia nyumba yake aliyoijenga kwa gharama kubwa na machozi yalianza kummiminika kama maji.
ITAENDELEA…………

Alsimama na kuamua kwenda kwa rafiki yake John ambaye alikua anakaa magomeni. Alikaribishwa ndani na mke wa rafiki yake huyo na kukutana na rafiki yake sebuleni kwake.
Walikumbatiana kwa kuwa siku nyingi walikuwa hawajaonana. Kwakua muda wa msosi ulikua unakaribia, mke wa John alipakua chakula na baada ya dakika kumi waliitwa kwenye meza ya chakula.

Walikula huku kila mmoja akijaribu kumuhadithia mwenzake yaliyotokea nyuma kwa kipindi chote hicho cha takribani miezi nane.
Jothan ndiye alikuwa wakwanza kumuhadithia mwenzake yaliyomkuta kuanzia safari yake ya Arusha hadi kufikia pale alipoenda kwenye nyumba yake na kukuta imeuzwa na mwanamke aliyekuwa anampenda na kumuamini kupita maelezo.

John alisikitika sana kuisikia story ile iliyomuumiza hata yeye.

“usijali rafiki yangu,. Kuhusu pa kukaa tu. Hapa umefika maana kuna vyumba vingi vya kutosha. Sasa vipi kuhusu docomments zako muhimu kama vyeti na vitambulisho vyako?” aliuliza John kwa kugundua umuhimu wa hivyo vitu.

“ndio maana nikakwambia kuwa nimechanganyikiwa sana. Yaani sijui nianzie wapi?” aliongea Jothan huku akionyesha wazi kuwa akili yake imeeshia pale kimawazo.

“usijali, vitapatikana tu.” Aliongea John na kuonyesha wazi nia yake thabiti ya kumsaidia rafiki yake huyo.

“vipi kazini, wameshamuajiri mtu mwengine wa kukaa katika nafasi yangu?” aliuliza Jothan huku akionyesha wazi kuwa na wasi wasi na nafasi yake ya kazi.

“mbona company imeuzwa kwa mzungu ambaye kaamua kuibomoa na kujenga hotel. We ukienda utaona tu mabati yamezunguka katika jengo la ofisi yetu. Sasa angalau ungekuwa na docoments zako zingekusaidia kupata malipo na mafao yako kutoka NSSF.”

Aliongea John na kumfanya Jothan ashike kichwa kwakua alikua anaamini kuwa maisha yake yanaweza kunyanyuka tena kama akivipata vitu vyake muhimu.

Kadi za benk, nyaraka mbali mbali na vyeti vyake alivyovihangaikia kuvipata ndivyo vilimnyima raha Jothan.

“mimi hivi sasa nimeajiriwa na kampuni ya Fast jet. Hata wewe ungekuwa na vyeti vyako tungekuwa tunafanya kazi wote . Maana watu wenye sifa kama zako wanahitajika sana pale.” Aliongea John na kumfanya Jothan ajiinamie.

Walikaa pamoja na baadae Jothan alielekezwa chumba atakachukuwa analala. Usiku baada ya kula chakula, alienda chumbani kwake Jothan na kulala.

Asubuhi ilipofika, John alimgongea Jothan na kumuaga. Alitoka na kwenda zake kazini.

Aliandaliwa chai Jothan na shemeji yake baada ya kuamka asubuhi na kutoka sebuleni. Alikunywa chai na kwenda chumbani kwake. Alioga na kubadilisha nguo.

“shemeji.. natoka kidogo.” Aliaga Jothan na kuondoka.

Alienda kinondoni ili kuangalia kuwa kama watu walionunua ile nyumba yake wameshahamia. Alikuta hali ile ile ya kama alivyoiacha.

Alijitahidi kumuulizia Shani kwa majirani wa pale, lakini hakuna hata mmoja aliyempa majibu chanya juu ya kumpata Shani.
Roho ilimuuma kila akiitazama nyumba yake. Alilia sana na kuamua kukubali yote kuwa hata kama atalia na kumaliza machozi yake, basi hawezi kuirudisha nyumba yake.

Alirudi nyumbani kwa rafiki yake aliye muhifadhi na kwenda chumbani kwake. Alikaa huko na baaae aliitwa na shemeji yake wakati wa chakula cha mchana. Walikula pamoja na rafiki yake aliwasili pale baada ya nusu saa.

“leo nimechelewa kurudi kwa sababu nilikuwa nashughulikia swala lako kwa kuvitangaza vyeti vyako kwenye magazeti mbali mbali yatokayo kesho.” Aliongea John na kumfanya Jothan afurahi kusikia hivyo.

Alikaa pale kwa wiki mbili zilizokwenda kwa amani. bada ya hapo, alianza kupata mitihani midogo midogo kutoka kwa Shemeji yake huyo aliyekuwa anapenda kumuonyesha tabasamu kila wakati.

Kadri siku zilivyozidi kusonga mbele, ndivyo majaribu kutoka kwa shemeji yake yalivyopamba moto hadi kufikia kuingia chumbani kwake akiwa na upande mmoja wa khanga nyepesi iliyoonyesha kila kitu alichokivaa ndani.

Alimuonya mara kadhaa lakini bado msichana huyo aliyekumbwa na pepo wa ngono juu yake alizidi kumuandama.

Kamwe hakupenda kuwa sehemu ya tatizo . Alipenda kuwa mtatuzi wa tatizo.

Baada ya kuona visa vinazidi kutoka kwa mke wa rafiki yake. Aliamua kuihama nyumba bila kumuambia rafiki yake sababu iliyomuhamisha pale nyumbani kwake kwa kuhufia kuharibu ndoa ya watu waliodumu kwa takribani miaka kumi. Japokuwa hakua na pa kwenda, ila aliamini kuwa kufanya vile basi Mungu atamnyooshea njia yake..

Fedha kidogo alizokuwa nazo zilimuwezesha kujihudumia mwenyewe na kulala gesti kwa wiki moja tu. Baada ya hapo alikuwa choka mbaya. Hakuwa na hata senti tano.

Siku hiyo aliamua kuuwa winga kwa kushinda na njaa hadi kiza kilipoingia. Hakuwa na mahali pa kulala, aliamua kwenda kukaa stendi ya daladala maeneo ya kinondoni huku akimuomba mungu usiku ule ukuche akiwa salama maeneo yale.

Masaa yalisogea na usiku mnene ulianza kutokea baada ya idadi ya magari kupungua huku watu waishio maeneo hayo kutoonekana nje.

Hata yeye mwenyewe hakujua alipataje usingizi. Ila alishtuka baada ya kuona mwanga mkali wa taa za gari ukimulika maeneo aliyokuwa yeye. Alishtuka na kuyazuia macho yake kwa mikono kutokana na ukali wa mwanga wa taa zile.

Sekunde kadhaa baadae, zile taa zilizimwa , mara akaona mlango unafunguliwa wa ile gari aina ya Range na kiatu aina ya high hills kikionekana kikikanyaga ardhi.

Hali hiyo ilimonyesha kuwa mtu ashukaye kwenye ile gari ni msichana. Uteke wa mguu ule pia ulimuwezesha Jothan kupima age ya mtu anayeshuka.

Wakati anausumbua ubongo wake kufikiria na kuwaza lengo la yule mtu kupaki gari lenye thamani pale, yule mtu alishuka na kufunga mlango.

Kutokana na mawenge ya taa, hakuweza kumuona mtu aliyekuwa akizihisabu hatua kuelekea pale alipo.
Yule dada alimsogelea mpaka pale. Hakuamini alichokiona mbele yake, alikuwa msichana wa ndoto zake toka alipokuwa anasoma. Hakujua ni kitu gani kilichomsukuma mpaka kufika maeneo yale. Ila aliamini kuwa ni Mungu pekee ndio amekisikia kilo chake na kuamua kuwakutanisha tena pale.

“PRISCA???””

Alinyaanyuka Jothan na kuita kwa mshangao mkuu huku akiwa haamini macho yake kuwa yule ndiye Prisca wake wa zamani.

Bila kujibu chochote, yule dada alianguka kifuani mwa Jothan huku machozi yanamtoka.

Hakuamini Jothan macho yake. Alimuangalia Prisca ambaye alikua anafuta machozi yake.

“tuondoke eneo hili, sio salama Jothan.” Aliongea Prisca na kumchukua Jothan na kwenda naye kwenye gari.

Safari ilianza huku kila mtu akiwa amenyamaza bila kuongea chochote. Jothan alishangaa kuona gari linaelekea mtaa aliokuwa anakaa yeye zamani kabla ya nyumba yake kuuzwa. Gari lilipiga honi kwenye geti la nyumba yake Jothan. Mlinzi alifungua mlango na Jothan hakuamini kuwa mmiliki wanyumba yake ni Prisca.

“siamini Prisca kama ni wewe ndio umeinunua nyumba hii?” aliongea Jothan baada ya kuingia kwenye nyumba ile ambayo haikubadilishwa kitu chochote zaidi ya rangi tu.

“siku zote huwa napenda kukuona ukiwa mwenye furaha. Ndio maana niliposikia nyumba hii inauzwa ndipo niliamua kuinunua kwa sababu sikupenda ipotee kwenye upeo wa macho yako. Sio nyumba tu, na kila kilichukuwa ndani pia nimevinunua. Hata gari lako pia ukilihitaji nitakupatia kwa sababu kwa sasa halipo hapa. Nimevinunua vitu vyote hivi kwa ajili yako Jothan.” Aliongea Prisca huku machozi yanamtoka. Jothan naye hakuweza kuyazuia machozi yake na kumfuata Prisca na kumkumbatia.

“moyo wa mtu ni kichaka Prisca, sikuweza kufikiria kama ipo siku Shani angeweza kuyabadili maisha yangu na kunifanya niwe hivi… nashukuru sana kwa yote uliyoyafanya kwa ajili yangu Prisca.”

Aliongea Jothan maneno yale na kumfanya Prisca azidi kulia.

“kesho nitachukua begi langu na kuondoka. Maana kazi yangu ya kukutafuta wewe nimeshaimaliza Jothan.” Aliongea Prisca na kumuangalia Jothan ambaye wote walikuwa wanalia wakati huo.

“hapana, hutakiwi kuondoka Prisca. Na kama utaondoka basi hii numba na kila kitu kilichomo humu ndani bado vitakuwa havitoshi kutimiza furaha yangu bila ya wewe kuwa karibu yangu.” Aliongea Jothan huku analia.

“mimi sio chaguo lako Jothan, siwezi kukaa karibu na wewe. Nitakuwa naumia roho tu na sitaweza kuvumilia kukuona ukiwa na msichana mwengine mbele yangu.” Aliongea Prisca huku analia kwa uchungu.

“nilikosea kuchagua kwakua sikujua upi ni mchele ni zipi ni pumba. Niliacha mchele kwakua pumba zilinivutia angi yake. Leo najuta kwakua pumba zimenilaza njaa. Wewe ndio mchele wa kunifanya nishibe na kunitoa njaa hii ya kufa inayonikabili. Nakupenda sana Prisca.” Aliongea Jothan na kujikuta ameeanguka kwa magoti mbele ya Prisca ambaye wakati huo na yeye alikuwa haoni vizuri kutokana na ukungu wa machozi ulikuwa kwenye macho yake.

“toka siku uliyonikana Jothan kule Peacock hotel kuwa mimi sio chaguo lako. Moyo wangu uliingia ganzi na kuamua kuishi single Jothan. Sihitaji tena kupenda kwakua nina bahati mbaya ya kupenda nisipopendwa. Sipendi kuumizwa tena kwakua maumivu yake siwezi kuyastahimili. Nikuache tu na maisha yako na mimi naiche na maisha yangu” aliongea Prisca kwa uchungu maneno yalimchoma sana Jothan ambaye bado alikuwa analowanisha viatu vya Prisca kwa machozi yake pale chini.
“nisamehe mimi, nimeshajifunza Prisca,” aliendelea kuomba Jothan huku sauti iliyojaa uchungu ikiendelea kumtoka mtoto wa kiume.

Nguvu ya mapenzi inaweza kuhamisha milima, wahenga walisema hayo na mimi nawaunga mkono kwa kusadiki maneno hayo.

Prisca alijikuta anamnyanyua Jothan na kumkumbatia. Wote walilia sana na kila mmoja kwa muda wake alimbembeleza mwenzake kwa mumfariji.

Ukurasa mpya wa mapenzi kwa wapendanao hao walioanza mapenzi toka walipokuwa shuleni yalianza kwa kasi kubwa.

Hakukua na sababu ya kuchunguzana wala kupeana muda. Walikubaliana kupima ukimwi kabla ya kufanya mapenzi.

Zoezi hilo lilifanikiwa kwa asilimia mia moja. Wote walikuwa wazima na mipango ya ndoa ilifanyika haraka.

Vitu vyote vilivyokuwa kabatini alivikuta vile vile. Kasoro hati ya nyumba tu ambayo alirudishiwa na mpenzi wake Prisca.

Alifurahi sana na kwenda kupeleka cv zake kwenye kampuni ya Fast jet. Alipata kazi haraka na kuungana na rafiki yake kipenzi John.

Ndoa ya aina yake ilifungwa kati ya Jothan na Prisca. Wageni wengi kutoka sehemu mbalimbali walihudhuria harusi ile.

Kwenye Hight table walikwepo John na mkewe, Bahati na mumewe Saimon pamoja na mama yake.

Hakika furaha ambayo ilipotea kwa muda mrefu kwa Jothan ilirudi alifurahia uwepo wa watu hao muhimu katika maisha yake kwa vipindi tofauti..

Miezi saba baadae, Jothan na mkewe Prisca walikuwa wanatoka kwenye matembezi yao usiku wa saa sita.

Wailpofika msasani. Walilakuta wasichana wengi walikuwa wamejiremba na kuvaa nusu uchi wakiashiria kuwa walikuwa wanauza miili yao.

Jothan hakuamini kumuona Shani akiwa amejiingiza kwenye kundi hilo. Alisikitika sana kumuona Shani akikimbilia magari na kuanza kujinadi kama wafanyavyo mada wengine wanaojiuza hapo.
Alisimamisha gari lake na kumuangalia mkewe ambaye alimpa ishara ya kuondoka na kumuacha mwanamke huyo na maisha yake.

Walirudi nyumbani na kumshukuru Mungu kwa kuwaunganisha tena na kuyahesabu yote yaliyotokea nyuma ni mitihani tu, na wao ndio couple iliyokubaliwa na Mungu.

***********MWISHO**************


Maisha ni sahani iliyojaa mazuri na mabaya. Kuna wakati unaweza kukubali kuwa maisha ni jinsi unavyoishi. Ila wapo wanaoishi nje ya malengo waliojiwekea. Hakuna anayependa kupata hasara, ila kama una muamini Mungu basi utaamini kuwa kupata hasara katika jambo Fulani ni moja ya mitihani na huenda mungu amekuEpushia kitu Fulani katika jambo hilo.

Kila hatua unayopitia ni moja ya changamoto katika mafanikio yako.

Ukianguka jikaze na jaribu kuruka tena hata kama utasikia maumivu. Tochi ya mungu hummulkika kila mtu isipokuwa kwa atakayekataa mwenyewe. Ridhiki ya mtu ipo kwenye mikono yake mwenyewe ndio maana huwezi kuizuia.

Mungu ametoa vitu vitatu vikubwa kuliko Mali.

Kwanza Mungu katoa akili za kipekee. Nikisema akili za kipekee namaanisha kuwa kila mtu Mungu kampa akili lakini hawa wenye akili za kipekee huweza kufanya mambo makubwa na ya kushangaza hali ambayo mtu uliyepewa akili ya kawaida huwezi kufanya hata kama una pesa.

Pili Mungu katoa vipaji. Mtu mwenye kipaji Fulani basi huweza kufanya mambo makubwa ikiwemo kufikisha ujumbe haraka kwa watu kutokana na kukubalika na watu wengi zaidi ya mtu wa kawaida.

Kimfano matangazo, tangazo hilo akipewa mtu Fulani atangaze basi muitikio utakuwa mdogo kuliko akipewa tangazo hilo Diamond, Mrisho Mpoto na wengne wengi.

Kipaji ni kitu cha pekee alichotoa mungu kama zawadi kwa mtu Fulani na kama kitathaminika na yeye kukiwekea mkazo basi hiyo ndio inaweza kuwa njia ya mafanikio yake kupitia kipaji hicho.

Tatu mungu katoa Moyo wa pekee. Moyo huu amewapa watu wachache. Na cha ajabu kuwa mtu mwenye moyo wa kutoa basi hutoa kitu kikubwa bila kujali kubakiwa na kidogo. Humshinda mwenye mali ambaye akitoa hata kitu kidogo huhisi anapungukiwa.

Mtu mwenye moyo wa pekee hupenda kutenda mambo yanayompendeza mwenzake hata kama yanaweza kuharibu furaha yake. Hapendi kumuona mtu akilia au akihuzunika wakati yeye anaweza kumfanya mtu huyo kuwa na furaha hata kwa kumuongopea. Hawezi kula yeye kabla ya kuangalia wenzake wenye njaa. Hayo na mengine mengi kajaaliwa mtu mwenye moyo wa pekee.

Na huwashinda wenye vipaji na akili za pekee. Watu hawa mungu huwajaalia kwa kuendelea kuwapa na kutia Baraka mali zao hata kama ni kidogo.

Nia na madhumuni ni kujifunza kupitia burudani hii iliyowaacha watu kwenye majonzi au kufurahia mwisha mzuri wa Jothan kuwa na mtu ampendaye.


MWISHO

Post a Comment

0 Comments