Header Ads Widget

Responsive Advertisement

UJUMBE MZITO KWAKO KIJANA


SIMULIZI FUPI - UJUMBE MZITO KWAKO KIJANA


Juzikati, mimi na washikaji zangu wawili, Ali na Hamisi tuliamua kwenda kumtembelea rafiki yetu fulani aitwaye Twaha ambaye alikuwa akisumbuliwa na magonjwa ya mara kwa mara.

Jamaa alikuwa akiishi Kimara, tulipofika kituoni, kwa kuwa tulikuwa na mapene, tukaona siyo kesi kama tukichukua bajaji, tukaiita na dereva akaja kutuchukua mpaka kwa kina Twaha.

Tulipofika kule na kuingia ndani, daah! Mshikaji alikuwa akiumwa, tulihisi kwamba ni ugonjwa wa kawaida, ila ile kumuona, kiukweli niliumia, machozi yakaanza kujikusanya mashavuni mwangu na baada ya dakika chache nikahisi yakianza kunitoka.

Niliumia, picha niliyoiona kitandani iliniogopesha. Twaha yule tuliyekuwa tukimuita Bonge, eti leo hii alikonda sana, yaani mwembamba mno, alikuwa akikohoa mara kwa mara na mwili kujaa vidonda. Tukamsalimia na kuanza kuzungumza naye.

TWAHA: Koh koh koh! Nimeamini huu ugonjwa upo. (Alizungumza kwa sauti ya chini)

MIMI: Ugonjwa gani?

TWAHA: Nyemo! Upo serious haujui nauzungumzia ugonjwa gani? Hebu niangalie, hivi mimi ndiye yule Twaha Bonge wa kipindi kile?

MIMI: Hapana! Ila hebu niambie, nini kilitokea?

TWAHA: Facebook! Instagram na Whatsapp!

ALI: Ilikuwaje Twaha?

TWAHA: Mnamkumbuka yule demu aliyekuwa akijiita Pretty Baby Gal Fetty?

MIMI: Namkumbuka, si ndiye yule mcute flani hivi?

TWAHA: Yeah!

HAMISI: Hahah! Tulimgombania sana, halafu ukatuzidi kete.

TWAHA: Mshukuruni Mungu! Nahisi matatizo yote yalianzia pale.

MIMI: Kwani ilikuwaje?

TWAHA: Yule demu nilimtokea, akaingia kingi ila baada ya kuwaponda sana washikaji zangu. Si unajua nilijua kwamba na nyie mnamlia misele, niliamua kuwaponda ili nimchukue. Naweza kusema kwamba mademu wote niliowahi kutembea nao, huyu manzi alikuwa mgumu sana. Nilichonga naye sana Facebook, alinipenda, akaniambia nikamfollow Instagram, nikaenda mpaka huko.

MIMI: Hivi alikuwa akitumia username gani Insta?

TWAHA: Nimesahau! Ila nilipomfollow kule, nikalike sana picha zake. Mwisho wa siku nikamuomba namba yake.

MIMI: Najua alikupa, ila ukatunyima.

TWAHA: Ndiyo ila haikuchukua muda mfupi kuipata, aliniletea pozi sana kwa kuniambia kwamba yeye alikuwa mtoto wa geti, nyumbani wazazi wakali, nikajiona nimepata, na kwa jinsi alivyokuwa akinikazia namba yake, nikaamini kweli alikuwa geti, kumbe siyo hivyo.

HAMISI: Ilichukua muda gani kupata namba yake?

TWAHA: Kama miezi miwili. Akanipa namba kwa masharti! Nisiwe nampigia usiku kwani atakuwa amelala. Kweli nikakubali. Huyu Fatuma alinichanganya sana.

ALI: Ikawaje?

TWAHA: Nilichati naye kwa kipindi kirefu, nikawa sioni wala sisikii kwake, nilimpenda na ndiyo maana kipindi kile niliwaambia nimepata stori demu malaya sana ili muachane naye, mliponiamini, mkaachana naye ili niwe peke yangu. Nilipokuwa nazungumza naye, sauti yake ilikuwa nyembamba mno, nzuri ya kumtoa nyoka pangoni. Sikutaka kukubali, niliamua kumfuatilia sana. Nikapanga kuonana naye! Alikuwa mgumu ile mbaya.

MIMI: Mmh!

TWAHA: Ndiyo hivyo! Miezi mitatu yote nikawa napanga kuonana naye, anakataa, ikaenda mpaka mwezi wa nne ndiyo akakubali, tena kwa masharti kwamba isiwe sehemu ya kificho, yaani twende sehemu ya wazi, nikaona haina noma, kweli nikaonana naye Mlimani City.

HAMISI: Ikawaje?

TWAHA: Nilipomuona, nikaamini kweli alikuwa mtoto wa geti, alivalia nikabu, baibui mpaka miguuni, nilichanganyikiwa na kuona kweli nimelenga palepale, nikasalimiana naye, tukafanya shopping kidogo na kuondoka zetu.

MIMI: Mlikwenda wapi? Gestinyo au?

TWAHA: Alinikazia siku hiyo, akasema kwamba muda bado, nilitakiwa kusubiri kwani ilikuwa mapema sana.

HAMISI: Mapema miezi minne yote?

TWAHA: Eti ndiyo hivyo! Nikaona usinitanie, nikaanza kumlazimisha, nikalazimisha na kulazimisha, nikawa kama natwanga maji kwenye kinu au kumpigia mbuzi gitaa, kila nikimwambia acheze, hachezi.

ALI: Ikawaje sasa? Yule demu alinizingua sana mpaka nikaogopa kwa kuona hapigiki.

TWAHA: Niiagana naye, akaondoka zake. Tuliendelea kuwasiliana zaidi. Hakunionyeshea tamaa, aliniheshimu, tena wakati mwingine akiona simu yangu ipo bize usiku, analalamika mpaka kulia. Nikahisi kama amechanganyikiwa kwa mapenzi yangu kumbe alisubiri niingie ndani ya 18 zake.

Siku zikasonga, mapenzi yakaniteka. Kuna siku aliniambia nimfuate sehemu fulani, kweli nikaibuka, kufika kule tukakaa na kunywa. Hakuwa akitulia na simu yake, mara aishike atume meseji, mara afanye hivi na vile, nilipokuwa nikiuliza, alisema kwamba mama yake alikuwa akisumbua. Kweli nikamuamini.

Siku hiyo nilikaa naye sana, baadaye akaniambia kwamba angependa apajue ninapoishi, nikaona yess....siku hiyo ndiyo ya kufanya yangu! Kweli nikaondoka naye. Alipofika hapa nyumbani, mtoto akapagawa, nikaona kama noma na iwe noma, siku hiyo hatoki, nikafunga mlango na ufunguo, kilichofuata, alisimulia magoli.

MIMI: Hahaha! Nacheka si kwa sababu napenda kucheka, ilikuwaje?

TWAHA: Nilihisi Fatuma mbichi, ila sikufichi. Kaka, nimechungulia mashimo mengi, simo lile, kama ni takataka, basi lile nalifananisha na la kule Mabibo.

HAMISI: Twaha! You are not serious my friend...Are talking about Fatuma I know or someone else?

TWAHA: Fatuma huyohuyo. Hakukuwa na msichana pale. Kiukweli aliniachia maswali mengi ila nikaona siyo kesi. Kuanzia siku hiyo nikawa napiga mdogomdogo.

ALI: Baada ya kila kitu ikawaje?

TWAHA: Mnakumbuka siku ile tuliyokwenda Maisha Klabu?

MIMI: Nakumbuka! Tena umenikumbusha! Kuna kipindi ulikuwa mnyonge sana, hivi nini kilitokea? Nilihisi kuna tatizo japokuwa ulitudanganya kwamba ulihisi unaumwa.

TWAHA: Kiukweli sikuwa naumwa. Siku ile nilikwenda kule kulipokuwa na njia ya kwenda Coco Beach. Nilimuona msichana kama Fatuma akiwa amekaa na wanaume wawili gizani huku sketi yake ikiwa mapajani.

MIMI: Twaha!

TWAHA: Nyemo! Niamini kaka.

MIMI: Ulimjuaje?

TWAHA: Unapokuwa umemzoea mtu, unamjua tu. Nilikuwa na uhakika kwamba alikuwa Fatuma. Nilirudi nikiwa na mawazo tele, nikaona haiwezekani, nikachukua simu yangu na kumpigia, kila nilipopiga, simu iliita lakini haikupokelewa.

MIMI: Unatudanganya.

TWAHA: Nyemo! Just look at me! Do I look like I’m joking.

MIMI: Nope!

TWAHA: Nilichanganyikiwa sana, niliumia moyoni. Baada ya saa moja nikarudi kulekule gizani, hawakuwepo. Nilinyong’onyea. Ilipofika saa nane akanipigia simu, harakaharaka nikaipokea. Akaniambia kwamba ameamka anakwenda chooni na ndiyo ameona missed calls zangu. Nikamuuliza alikuwa wapi, akanijibu alilala.

ALI: Mmmh! Nina uhakika ulimfananisha.

TWAHA: Sidhani! Sikuwahi kumfananisha Fatuma. Aliniambia kwa maneno matamu mpaka ishu ya kule gizani nikaisahau. Sasa siku moja nilimfuata chuoni kwao kwa kushtukiza. Nilimuulizia nikaambiwa alifuatwa na mwanaume chuo, alikuwa na VX mpya kabisa. Kiukweli nilichanganyikiwa, nikaona nadanganywa. Nikampigia simu, akaniambia kwamba kaka yake alimfuata kumrudisha nyumbani. Nikamuuliza kweli alikuwa nyumbani, akaniambia kwamba wamepitia kwa mama yao mdogo, baada ya hapo watakwenda msikitini kuswali kisha kwenda kwenye Maulidi.

MIMI: Aisee! Lete maneno.

TWAHA: Alivyoniambia hivyo! Moyo wangu ukapoa, hasira zikapungua, wivu ukanitoka, nikakubaliana naye. Kuanzia siku hiyo nikawa nimeongeza mapenzi si unajua kumpata msichana aliyeshikilia dini ni adimu. Nikapagawa.

MIMI: Unazunguka sana, lengo la kutuambia haya ni nini Twaha?

TWAHA: Kuna mengi sana yalitokea ila nilikuja kujua ukweli baada ya siku kunitembelea gheto, aliiacha simu yake na kwenda chooni. Nikaitazama simu ile na kutoa pattern kwa kukiangalia kioo na kuona mchoro. Nikakutana na meseji zaidi ya 20 za wanaume whatsapp, tena zote zikionyesha kwamba wote wameshampitia. Nilichanganyikiwa.

HAMISI: Pole sana. Ikawaje.

TWAHA: Niliumia, nikapoa, sikumwambia. Nakumbuka kuna meseji moja iliandikwa kwamba wakutane Hong Kong Bar saa tano usiku, nikaikariri meseji hiyo. Saa tatu tu nikafika Hong Kong Bar, nilitaka kuhakikisha. Kweli, saa tano nikamuona Fatuma akija, mavazi aliyovaa ni vigumu kumtofautisha na changudoa. Nikajiuliza kweli yule alikuwa Fatuma mwenyewe au nilikuwa naota. Nikaona haiwezekani, nikampigia simu, nikaona simu yake ikiita, akakiangalia kioo kisha akaiweka pembeni. Niliumia sana.

Baada ya dakika kadhaa, nikaona mwanaume mmoja akitokea hapohapo na kumchukua na kwenda naye pembeni kabisa kwenye giza. Nikabaki nikimwangalia kwa hasira. Kumbe wakati namwangalia hivyo, kuna mhudumu aliniona, akanifuata na kuanza kuzungumza naye.

Akaniambia kama namtaka Fatuma niseme aniitie halafu nimtoe na shilingi elfu kumi kishikaji. Nikamwambia demu ni kweli mkali, ila kuna la zaidi? Akasema hakuna jingine ila demu ni muuzaji sana pembezoni mwa baa hiyo yaani kama namtaka, pesa yangu tu kwani watu wengi wanajipigia.

MIMI: Twaha! Unamaanisha Fatuma huyuhuyu?

TWAHA: Ndiyo!

MIMI: Huyuhuyu tuliyekuwa tukimgombania?

TWAHA: Ndiyo!

MIMI: Si huyuhuyu mwenye picha zote akiwa amevalia hijabu na baibui?

TWAHA: Nyemo! Ndiye huyohuyo. Nikamwambia jamaa aniitie, nikamtoa na elfu kumi. Kumbe kule alipokuwa ni sehemu ya kufanya ngono. Ni kiwanja alichokizoea, jamaa akaniambia nisubiri. Baada ya saa moja, nikamuona akitoka na mwanaume yule kuondoka. Jamaa akaenda kuniitia. Kweli akaja.

HAMISI: Ikawaje, alitamani kukimbia?

TWAHA: Atamani kukimbia? Kakudanganya nani? Aliponiona, akaonyesha tabasamu kisha akaniambia kama nahitaji huduma. Yaani hapo palikuwa kazini kwake, hivyo mambo ya ubaby baby nisubiri nyumbani. Nilichanganyikiwa sana. Nililalamika, mno, walinzi wa pale wakaja, wakanitoa mkuku.

Kuanzia siku hiyo ndiyo ukawa mwisho wangu na yeye. Nilipokwenda kule mtaani kwao na kuulizia tabia zake, nikaambiwa huwa anajiuza na wao majirani walishangaa kuona nikiwa nimekufa na kuoza kwa changudoa.

Nilihuzunika sana na ndiyo nikaamua kwenda kupima, nikajikuta nimeathirika. Yaani Fatuma aliniambukiza UKIMWI.

ALI: Pole sana Twaha!

TWAHA: Asante sana. Yaani imeniuma sana. Wakati mwingine natamani kurudisha muda nyuma, nirekebishe nilipokosea ila ndiyo hivyo, haiwezekani tena. Moyo wangu unaniuma sana.

Humu facebook, Insta na Whatsapp si pa kumuamini sana mtu, usibabaike na mwanamke anayejistiri ukahisi kwamba ndiye msafi, usibabaike na msichana aliyepiga picha huku kashika Biblia ukajua ndiye anaijua dini, humu kwenye mitandao ya kijamii panatisha ndugu zangu.

Nyie mlikoswakuoswa ila nimepatwa mimi. Kuweni makini, inawezekana kupatwa mimi lilikuwa dhumuni la kuwaambia nyie kwamba UKIMWI upo. Kifo ni kifo lakini cha UKIMWI kinatesa sana. Ndugu zangu, huu ni muda wa kubadilika, si muda wa kurukaruka kila kona, sehemu nyingine ni hatari.

Alimalizia Twaha huku akilia kama mtoto. Kazi yetu ikawa ni kumbeleza. Mbali na Fatuma huyu wa Twaha! Amini kwamba kuna wengi kwenye mitandao ya kijamii ambao kazi yao ni kukatisha ndoto za watu.

Si kwa wanawake tu, hata wanaume wapo. Ni wasafi kwa kuwaangalia, ni watanashati lakini nyuma ya pazia, wana maisha ya kutisha, cha msingi tubadilike, tusikatishwe ndoto zetu kwa sababu ya starehe ya dakika moja tu.

Post a Comment

0 Comments