Header Ads Widget

Responsive Advertisement

MDUDU ALINIUMA



 MDUDU ALINIUMA

Mbinguni, jua lilikuwa limemaliza kazi yake na sasa lilijikokota magharibi huku mionzi yake miekundu ikiwapungia walimwengu kwa ulegevu kana kwamba kuwashukuru wale wote walioipenda. Masikini nilibaki pale uani nimelitumbulia macho, huku machozi yakijikusanya tayari kumwagika. Heri ningekuwa jua. Nisingekuwa na wasiwasi wa swala lolote. Langu lingekuwa tu kuchomoza asubuhi na kutua jioni.

Nilikuwa nimechoka kuwatazama wapita njia na magari ya kifahari. Yalikuwa mapya na yalikwenda kwa kasi tena bila kutoa sauti. Lakini kuna yale yaliyochakaa yenye breki zilizokwaruzana kila yaliposimama. Watu nao walipita wa aina tofautitofauti; si weusi, si weupe, warefu kwa wafupi na hata vijana kwa wazee. Kwa umbali,taa za umeme zilikuwa zimelimwaia jiji mchana bandia wa mwangaza. Ishara kuwa usiku ulikuwa unaingia na giza kuanza kutawazwa.
Yote hayo sikuyaonea fahari tena. Mambo yalikuwa kangaja kumbe na sasa yalikuja. Niliketi nikiwazia matokeo ya daktari, ambayo niliyapokea takribani miezi miwili iliyopita. Awali, walinificha ukweli lakini niliposisitiza, nilipasuliwa mbarika. Laiti wasingelinijuza kwani tangu hapo maisha yangu yalichukua mkondo tofauti mno. Mwenyewe, ile hamu na tama ya kula vyakula iliniondokea. Nikawa sili lolote, sinywi chochote. Mashavu yangu yalizidi kushobwekea ajabu. Nguo zangu ningezivua, mbavu zingehesabika hadharani moja baada ya nyingine. Nyele zangu zilizokuwa ndefu na nyeusi ti sasa zilibadili rangi na kuanza kuchipuka ovyoovyo. Mdudu alikuwa ameniuma. Lakini yupi?


Darubini yangu ilinikumbusha mambo yalivyoanza. Yote yaling’oa nanga baada ya kumaliza kidato cha nne. ‘Mrembo’ nilijidai kwenda jijini kutafuta kazi ya ukarani. Niliwahakikishia wazazi kuwa nilikuwa na rafiki wengi waliojitolea kunipa makao wakati nikitafuta kazi. Wavyele wakadinda kuniruhusu mwanzoni lakini baada ya kuzidi kusisitiza na kufanya kiburi nyumbani, waliafikiana na kuniacha kwenda zangu. Pengine walikumbuka kuwa mtoto akililia wembe mpe. Nilipokuwa nikiondoka, mama alikuwa na huzuni mno na kwa uchungu, alinionya kuwa mwenda tezi na omo marejeo ni ngamani. Potelea pote. Sikutaka kusikia ya yeyote kwani nilijitia hamnazo nisikie la mwadhini wala la mteka maji msikitini. Nikawa binti kiziwi asiyesikia anayoambiwa.
Kazi baada ya kuikosa,nilijiunga na wenzangu na tukajiajiri wenyewe. Malipo yakawa ya kuvutia ajabu kwani wateja walivyoongezeka ndivyo malipo yalivyoongezeka. Alimradi ujue namna ya kuwaongelesha na kuwahudumia wateja sawasawa. Jambo ambalo nilijifunza kufanya hata nikabobea na kutopea katika nyanja hiyo. Waume niliwabadili kama nilivyobadili mavazi yangu kwa siku. Nikawa ndiye jogoo la shamba lililowika jijini. Nikazika katika kaburi la sahau kuwa jijini kuna papa na papaupanga, ambao ukiwapapia, hukosi kupapatika kwa majuto, dhiki na mateso kama hayo yaliyonikumba sasa. Lau kumbe mwiba wa kujidunga hauna kilio.


Kutoka hapo uani nilikoketi, taa za umeme nilizoziona zilinikumbusha mengi. Kuhusu mienendo yangu ya awali nilipokuwa kipusa ajabu. Niliingia kwa vilabu hivyo vyote vya usiku huku mikono ya watu tofauti yamezinga kiuno changu chembamba kama cha nyigu. Daima kucha zangu zilizokuwa ndefu na zilinaksishwa rangi sawia na nguo zilizovalika.  Mdomo wangu ukakolezwa rangi nyekundu kana kwamba nililamba damu mbichi. Lakini kumbe dunia mti makavu kiumbe usiuegemee.
Watu hao niliowatazama waliniongezea uchungu mtupu. Moyo wangu mchanga ulijaa uchukivu na furaha ikawa imeyeyuka kama kipande barafu katika utupu wa mchanga wa jangwa la Sahara. Wale wasichana warembo waliovalia mavazi yaliyoacha sehemu za miiliyao kuonekana waliniudhi zaidi. Laiti wangelijua kuwa dunia itawararua na kuwaacha uchiuchi, wasingefika hata barabarani. Nilitamani kuwafikia niwaonye na kuwapa ukweli wa mambo kuhusu madhara ambayo yangewasibu lakini nilishindwa. Mimi pia nilikuwa hivyo na sasa nilikuwa naangamia. Nikakumbuka kuwa asiyefunzwa na mamake hufunzwa na ulimwengu.
Waume nao niliwatazama kama wanyama mwitu waliovalia suruali ndefu na sharti tofauti. Wanyama wenye uwezo mkali wa kukuvamia wakakumaliza kabisa. Wao ndio walionipa maji machafu yaliyokuwa na mdudu ambaye aliniuma na kunifanya kuugua sasa. Niliwatazama kwa uchukivu mwingi.


Raha nyingi ya ulimwengu ulitoweka na badala yake ikawa sasa ni huzuni tupu na majuto. Sasa niliishi kwa jumba hilo kubwa peke yangu. Ulimwengu ulinitenga kana kwamba mwenye ukoma. Wale wote waliokuwa wakiingia na kutoka siku nzima hata usingewaona. Dada yangu mdogo ndiye alijitolea kuniuguza pale kwani sikutaka kuishi na wazazi na kuwapa mzigo wa kunitunza. Ikanijia kuwa mla nawe hafi nawe ila mzaliwa nawe. Sikujua wa kumlaumu. Wazazi? La wao walinitakia mema na kunionya kusoma kwa bidii. Marafiki? Kwa kiasi kidogo lakini ndimi niliyekubali kudanganywa. Ulimwengu? Ndiyo lakini sehemu gani ya ulimwengu? Mimi ndiye wakulaumu na sasa mwiba wa kujidunga hauna kilio.


Ndoto zangu zote zilitoeka kama ukungu na umande. Azimio langu la kutaka kuendeleza masomo katika chuo kikuu katika fani ya sheria, na kufuzu katika uzamifu na uzamili lilitoweka ghafla kama mwangaza wa mshumaa uliozimwa na upepo. Nilitoka uani na kuingia katika chumba changu cha kulala. Mezani, kulikuwa picha yangu ya awali.nilijiangalia tena na kujiona tofauti; mnene, mwenye sura ya maji ya kunde tena mcheshi ajabu. Lakini sasa nilikuwa kama shetani hata ingawa sijawahi kuonana naye ana kwa ana. Haina maana kuishi katika hali hiyo! Niliifikia kalamu na kuandika kitu kwa karatasi iliyokuwa hapo kando. Kasha nikavuta kijichupa kilichokuwa hapo juu na kupiga makopo kadhaa ya yaliyokuwemo. Maini ya kaanza kukeketeka na koo kuungua ndanindani. Heri nife niiondokee dunia. Safari yangu ya kuenda jongomeoni ikawa imeanza nilikolala sakafuni.
Niligutuka usingizini nikihema na kutweta kwa nguvu mno hata nikashindwa kuendelea kulala. Ilikuwa ndoto ya ajabu.

MWISHO

Post a Comment

0 Comments