Header Ads Widget

Responsive Advertisement

MALIPO NI HAPAHAPA



 SIMULIZI FUPI : MALIPO NI HAPAHAPA

Katika Mji wa Arusha Mtaa wa Kaloleni ni eneo ambalo wakazi mbalimbali walipendelea sana kuishi kutokana na mazingira yake kuwa tulivu na yenye mandhari nzuri. Katika mtaa huo aliishi mzee mmoja aiitwaye Magesa. Mzee huyo alikuwa na mke na watoto watatu, watoto wawili wakiume ambao waliitwa Joseph na Peter na mtoto mmoja wa kike aliyeitwa Julieth.

Mzee Magesa hakuwa na uwezo mkubwa sana kifedha. Maisha ya Mzee huyo na famila yake yalitegemea sana kipato kidogo kilichotokana na biashara ya kuuza mboga sokoni ambayo alikuwa anaifanya siku zote za maisha yake hadi akapewa jina la ‘Muuza mboga’. Mke wake alikuwa ni mama wa nyumbani akijishughulisha na kupika chapati na kuuza ili kuongeza kipato kwa ajili ya mahitaji ya pale nyumbani.

Maisha yalikuwa magumu sana lakini familia ilikuwa na furaha na upendo kwani waliishi kwa kupendana na kuheshimiana. Mzee Magesa aliwapenda sana watoto wake, kwani mara nyingi alikuwa akiwafundisha mambo mbalimbali kuhusu maisha ikiwa ni pamoja na kuwasisitiza kusoma. Julieth alikuwa Darasa la Tano na mdogo wake Joseph alikuwa Darasa la Pili, Peter yeye alikuwa hajaanza shule.

Siku moja yapata saa mbili usiku Mzee Magesa akiwa amekaa kwenye sebule karibu na chumba chake cha kulala alimwita Julieth kwa ajili ya mazungumzo.
“Julieth!” Mzee Magesa aliita kwa nguvu. “Abee baba!” Aliitikia Julieth aliyekuwa anaosha vyombo huku akimwendea baba yake.
“Unafanya nini saa hizi?” Mzee Magesa aliuliza kwa sauti ya upole.
“Naosha vyombo baba.” Alijibu Julieth kwa adabu.
“Umemaliza?” Aliuliza tena Mzee Magesa.
“Hapana baba, bado sufuria mbili.” Alijibu Julieth.
“Acha utamalizia kesho kaa hapo nina maongezi na wewe.” Aliongea Mzee
Magesa huku akinyoosha kidole kwenye kiti cha miguu mitatu.
“Nimekuita ili kukwambia maneno machache kuhusu hali ya maisha yetu
hapa nyumbani.” Mzee Magesa alianza kueleza sababu ya wito huku
Julieth akimwangalia na kumsikiliza baba yake kwa makini.

“Kama unavyoona hali yetu ya maisha tunayoishi ni ngumu sana. Na hii
inatokana na kipato chetu kuwa kidogo. Namna pekee ya kujikwamua na
hali hii ni wewe mtoto wetu mkubwa kusoma kwa bidii ili uje utusaidie
sisi wazazi wako pamoja na wadogo zako. Na pia …” Mzee Magesa
alikatisha ghafla huku akiwa kama amekumbuka kitu fulani muhimu.
“Mama yako yuko wapi?” Aliuliza Mzee Magesa.
“Yupo chumbani.” Alijibu haraka Julieth.
“Mama Julieth!” Aliita Mzee Magesa.
“Abee!” Aliitikia mama Julieth kutokea chumbani huku akitoka.
“Mama Julieth nina maongezi kidogo na Julieth naomba na wewe
ushiriki.” Alitamka Mzee Magesa.
“Maongezi gani hayo?” Aliuliza mama Julieth.
“Wewe kaa usikilize ndio maana nimekuita”. Mzee Magesa alijibu kisha
akaendelea kuongea na Julieth huku mama yake akiwa amekaa pembeni
mwa Mzee Magesa.
“Julieth kama nilivyoanza kukwambia maisha yetu ni magumu sana
kutokana na kipato kidogo tunachopata. Tumejaribu kufanya bidii lakini
hakuna mabadiliko. Njia pekee ya kujikwamua kiuchumi katika siku zijazo
ni elimu. Hivyo wewe kama mtoto wetu mkubwa unatakiwa usome kwa
bidii sana ili uje utusaidie sisi na wadogo zako pia. Sisi wazazi wenu
tutakazana kuhangaika kutafuta fedha ili wewe usome. Angalia Mzee
Mtokambali alisomesha mtoto wake wa kwanza hadi Chuo Kikuu, leo hii
wadogo zake mmoja yupo Kidato cha Sita na mwingine Chuo Kikuu.
Maisha ya Mzee Mtokambali ni mazuri. Ninaimani hata sisi hili
linawezekana ilimradi tu kama wewe una nia ya kusoma.”
“Ni kweli angalia mke wake anavyobadilisha kanga na vitenge, ni kutokana
na kijana wao mwenye kazi nzuri. Baba Julieth, hili linawezekana mbona
binti yetu ana nia sana ya kusoma na uwezo anao.” Alidakia mama Julieth
bila hata kusubiri Mzee Magesa amalize.

“Baba na mama nimesikia sana mawazo yenu mazuri ninapenda sana
kusoma. Nitasoma!” Alisisitiza Julieth. “Julieth wewe ndiye binti yetu wa kwanza, kumbuka wadogo zako bado ni wadogo sana nakuomba mwanangu siku zote za maisha yako mtu asikudanganye ukawachukia wadogo zako. Uwapende ndugu zako na kuwaheshimu watu wote wanaokuzunguka wakubwa kwa wodogo, kwani mwanangu kuna leo na kesho leo mimi na mama yako hatutakuwepo mshikamano na upendo ndiyo silaya yenu.

Hata ukisoma sana kama hutawapenda na kuwaheshimu wadogo zako na watu wote itakuwa ni bure.” Aliongeza Mzee Magesa. Julieth aliinamisha kichwa chini kama vile anatafakari kitu halafu akawaangalia baba na mama yake kwa uso wenye maswali. “Baba mbona mnaongea hivi? Mimi nawapenda wadogo zangu na watu wote, hata siku moja haitatokea nikawachukia wadogo zangu. Lakini mbona leo mnaongea hivi?” Aliuliza Julieth kutaka kudadisi zaidi.
“Huu ni mwendelezo tu wa maongezi ambayo mara kwa mara mimi na mama yako tumekuwa tukifanya. Ila leo tumeongea kwa msisitizo zaidi kwani maisha ni magumu kupita siku zilizopita. Lakini pia kumbuka sasa umekuwa mkubwa hivyo lazima tukwambie msimamo wetu juu ya maisha yetu, yako na ya wadogo zako, au siyo mama Julieth!” Alifafanua Mzee Magesa huku akimgeukia mama Julieth. “Ni kweli wewe ndo mkubwa lazima uyajue haya kuanzia sasa ili kukujengea uwezo wa kuishi vizuri na watu.” Aliongeza mama Julieth. “Sawa wazazi wangu nimewaelewa.” Alisema Julieth.
“Baba Julieth naona tumalize maongezi kwani kesho asubuhi na mapema
unatakiwa uwahi sokoni kufungua biashara. Na wewe Julieth kesho ni
shule, hebu tukalale.” Alishauri mama Julieth.

“Haya Julieth nenda kapumzike ila ukae nayo kichwani yote
tuliyozungumza leo.” Alisisitiza Mzee Magesa huku akisimama kuelekea
chumbani.
“Sawa baba.” Alijibu Julieth.

Kesho yake asubuhi waliamka mapema sana. Julieth alijiandaa haraka na kunywa uji na kuwahi shuleni. Mzee Magesa aliweka mboga zake kwenye mkokoteni na kuelekea sokoni. Mama Julieth tayari alikwishaanza kupika chapati kama kawaida yake. “Mke wangu leo nitachelewa kurudi kwani nikifunga tu biashara itabidi niende kuchukua vitunguu na nyanya. Ninaomba leo usiku unipikie ugali na matembele.” Aliomba Mzee Magesa huku akiondoka na toroli lake kuelekea sokoni.“Haya baba kazi njema ila sio ndiyo uchelewe sana, halafu usisahau kuleta matunda.” Aliongea mama Julieth huku akimsindikiza kwa macho.

Mzee Magesa alipofika karibu na sokoni akiwa anavuka barabara, ghafla lilitokea gari likiwa katika mwendo wa kasi ya ajabu na kumgonga. Mzee Magesa aliumia sana sehemu za kichwani na sehemu mbalimbali na kusababisha kutoka damu nyingi mdomoni, puani na masikioni.Wasamaria wema walimkimbilia Mzee Magesa ili kumwahisha Hospitali ya Mkoa lakini alikufa palepale hata kabla ya kuondoka.

Mashuhuda wa ajali walijaribu kuchukua namba za gari lakini haikuwa rahisi kwani halikusimama. Walipiga simu polisi na askari walifika baada ya muda wa kama dakika ishirini hivi. Baada ya kuwahoji walioshuhudia ajali ile waliuchukua mwili wa Mzee Magesa na kuondoka. Baada ya askari kuupeleka mwili wa marehemu Hospitali ya Mkoa askari wawili walikwenda kutoa taarifa nyumbani kwake. Walipofika walimkuta mama Julieth katika biashara yake ya chapati. “Habari yako mama.” Askari mmoja alisalimia. “Nzuri tu karibuni.” Alijibu mama Julieth na kuwakaribisha akidhani ni
wateja wake wa chapati.

“Asante mama sisi ni maofisa usalama tumekuja kukupa taarifa kwamba mume wako amepata ajali.” Wale askari walizungumza moja kwa moja kitu ambacho kilimpa mshtuko mama Julieth na kushindwa kuamini alichoambiwa na kabla hawajaendelea mama Julieth aliwakatisha. “Nini? Jamani mbona siwaelewi, mume wangu amepata ajali wapi? Na ya nini? Je, hali yake inaendeleaje?” Aliongea mama Julieth maneno mengi kama mtu aliyechanganyikiwa. “Amegongwa na gari na kwa bahati mbaya gari halikusimama.” Askari alifafanua.

“Mbona mnazunguka nimeuliza hali yake iko vipi?” Mama Julieth aliendelea kuhoji zaidi huku ametoa macho mithili ya panya aliyebanwa kwenye mtego wa chuma. Wale askari wakatazamana kwa sekunde chache kisha mmoja wao akatamka. “Wewe ni mwanamke lakini tunakusihi ujikaze kiume.” Akamwangalia usoni mama Julieth kisha akaendelea.
Mume wako yupo katika Hospitali ya Mkoa katika chumba cha …” “Wagonjwa mahututi?” Mama Julieth alimalizia sentensi akiwa kama aliyechanganyikiwa. Askari kuona hali ya kuchanganyikiwa kwa mama Julieth akaamua
kumdanganya.

“Ndiyo mama yupo ICU. (Intensive Care Unit)” Alifafanua Askari. “ICU? Ndo wapi huko mbona unanichanganya.” Alihoji mama Julieth. Samahani mama ninamaanisha yupo chumba cha wagonjwa mahututi anafanyiwa uchunguzi wa kina. Kisha mama Julieth aliwaomba wale askari ajitayarishe ili aongozane nao. Baada ya dakika kama tano hivi mama Julieth alikuwa tayari kuelekea kumwona Mzee Magesa. Walipofika askari mmoja aliwaambia wasubiri kidogo nje ili akamwombe daktari ruhusa ya kumwona mgonjwa.

Askari mmoja alibaki na mama Julieth katika chumba cha mapokezi huku yule mwenzie akiingia katika chumba cha daktari ambaye ndiye aliyepokea mwili wa Mzee Magesa na kuthibitisha kitaalamu kwamba kweli Mzee Magesa alikuwa amekufa. Daktari aliposikia kutoka kwa askari kwamba mke wa marehemu amekuja alimwambia akamwite. Haraka askari alitoka nje na kuwakuta wakimsubiri kwa hamu na kutoa ishara ya kumfuata. Wote walielekea ofisini kwa daktari. “Karibuni mkae kwenye viti”. Daktari alitamka kisha akaendelea huku akimwangalia kwa makini yule mama. Kwa bahati mbaya alifikiri wale askari walikwisha mwambia kuhusu kifo cha Mzee Magesa.

“Pole sana mama mwili wa mumeo upo katika chumba cha …..? Kabla ya kumaliza kusema mama Julieth alianguka chini na kupoteza fahamu. Haraka wale askari walimbeba Mama Julieth na kumwingiza katika chumba maalumu ambako alipata huduma na kupata fahamu baada ya saa 3. Kisha daktari aliwaomba wale askari kumsindikiza mama Julieth nyumbani kwake.

Majirani zake mama Julieth walikwisha kusanyika nyumbani huku mmoja
wao akienda shuleni kuwafuata watoto. Baada ya kufika mama Julieth vilio
na kelele za kila aina vilitawala huku mama Julieth akianguka chini na
kukosa nguvu kabisa. Mipango ya mazishi ilifanyika na kuamua kuzika
siku iliyofuata.
Siku ya mazishi watu walijaa sana huku simanzi na masikitiko vikitawala
katika eneo lote la Kaloleni kwani Mzee Magesa alikuwa maarufu sana.
Mwili wa Mzee Magesa ulizikwa kwa taratibu zote huku viongozi wa dini
na serikali kutoka Kaloleni wakihudhuria na kutoa nasaha zao. Huo ndio
ulikuwa mwisho wa maisha ya Mzee Magesa ‘Muuza mboga’ sokoni.
Wiki mbili baada ya mazishi Mama Julieth alikuwa bado hajapata nguvu
za kuanza kufanya chochote. Siku moja alikuwa amekaa katika ngazi
amejiinamia kama mtu ambaye amekata tam aa ya maisha, akiendelea kulia
kwa uchungu. Julieth alitoka ndani akiwa ameshika kikombe cha chai na
kumpa mama yake huku akimfariji.
“Mama usilie, sisi tupo na wewe Mungu atatusaidia.” Julieth alimfariji
mama yake huku akimpa chai.
“Mwanangu baba yenu alikuwa nguzo ya familia na sasa hayupo tena.
Kumbuka mnatakiwa msome nani atawasomesha? Hivi ni kwa nini
Mungu amemchukua mapema hivi?” Alijibu mama Julieth huku
akibubujikwa na machozi.
“Mama tusikate tamaa hata baba kabla hajafariki alisema tuwe na
mshikamano na upendo katika familia yetu. Mama mimi nitakuwa nawe
bega kwa bega kukusaidia.” Julieth aliendelea kumfariji mama yake.
Mama Julieth alimwangalia Julieth kwa macho ya matumaini kisha
akamkumbatia mwanawe.
“Sawa mwanangu kwani yote haya ni mapenzi ya Mungu.” Alijibu mama
Julieth na kuanza kunywa chai.
Basi Julieth aliendelea na kazi za ndani na kumwacha mama yake akiwa
amepumzika.
*************
Baada ya mwaka mmoja kupita tangu Mzee Magesa afariki mama Julieth
aliugua ugonjwa wa moyo, kwa hiyo akashindwa kuendelea kufanya kazi
zake za kila siku na hata biashara ya sokoni aliyokuwa akiifanya baba
Julieth hakukuwa na mtu wa kuwasaidia kuiendeleza. Hali ya kipato ilizidi
kuwa ngumu kutokana na kuugua kwa mama Julieth kwani hata kazi ya
kupika chapati hakuweza kuendelea nayo tena.
Kutokana na hali ya maisha kuzidi kuwa ngumu Julieth aliamua kuacha
shule akiwa Darasa la Sita ili kumsaidia mama yake kazi za pale nyumbani
na ikiwa ni pamoja na kuuza chapati.
Julieth alianza kuuza chapati biashara ambayo haikuwapa kipato kikubwa
kuweza kujikimu kutokana na wateja kuwa wachache. Kutokana na maisha
kuwa magumu walilazimika kula mlo mmoja kwa siku ili kukusanya kodi
ya vyumba viwili walivyokuwa wanaishi. Julieth aliendelea kuvumilia bila
kukata tamaa kwani mbali na kuwa ni binti mdogo lakini alikuwa na
majukumu makubwa ya kutunza familia.
Katika kuuza chapati Julieth alikutana na watu mbalimbali waliozipenda
sana chapati alizokuwa akipika. Siku moja asubuhi alikuja kaka mmoja
kununua chapati akatokea kumpenda sana Julieth.
“Habari yako mrembo!” Yule kijana alimsalimia Julieth huku akitabasabu.
“Nzuri kaka karibu.” Alijibu Julieth huku akimwangalia usoni.
“Mimi naitwa John sijui mwenzangu unaitwa nani?”Alijitambulisha yule
kijana.
Julieth alisita kidogo halafu akajibu;
“Naitwa Julieth karibu kaka chapati shilingi mia moja na hamsini nikupe
chapati ngapi?” Alijibu Julieth.
“Naomba chapati mbili.” Alitamka John huku akimpa noti ya shilingi elfu
kumi.
“Mmh jamani huna hela ndogo kaka au kuna kitu kingine unataka
kununua dukani nikakuchukulie, asubuhi hii chenchi zinasumbua kweli.”
Alisema Julieth kwa kulalamika.
“Usijali Julieth nipe hizo chapati na fedha inayobaki ni zawadi yako.”
Alijibu John.
“Mh we kaka, hela yote hii nibaki nayo kuna usalama kweli? Hapana kaka
ngoja nikutafutie tu chenchi.” Alisema Julieth huku akinyanyuka kwenda
dukani.
“Julieth usiogope mimi sina nia mbaya na wewe chukua tu hiyo hela
itakusaidia usijali.” Alitamka John huku akimzuia kuondoka.
Julieth aliamua kukaa chini na kumsikiliza John hatimaye wakafahamiana.
John alikuwa ni mkazi wa Mwanza na alikuwa ni mfanyabiashara wa
samaki. Julieth alimweleza hali halisi ya maisha yao. Baada ya kufahamiana
kwa siku kadhaa walianza kuwa marafiki na baadaye John alimtaka Julieth
awe mpenzi wake. Mwanzoni Julieth alikataa sana kuhusu urafiki wa
kimapenzi na John. Lakini baadaye alikubali wakawa marafiki. siku moja
Julieth akiwa amekaa nje ya nyumba yao John alipita pale na kufanya
maongezi na Julieth.
“Julieth tumekuwa marafiki kwa muda wa wiki tatu sasa naona nikwambie
ukweli. Kutoka siku ya kwanza nilipokuona nilitamani sana uwe mpenzi
wangu. Naomba unipe nafasi ndani ya moyo wako. Nakupenda Julieth
zaidi ya urafiki tulionao.” John alimwambia Julieth.
“Haiwezekani John! Mimi ni masikini sana unaiona familia yetu
inanitegemea sana mimi, halafu nianze tena mapenzi! Hapana! Tena sitaki!
Wewe tafuta tu mwanamke atakayekufaa anayeendana na wewe.” Alikataa
Julieth kwa msisitizo mkubwa.
“Sikiliza nikwambie Julieth, mimi na wewe tukiwa pamoja hata familia
yako itakuwa yangu pia, tutasaidiana sana katika maisha. Mama yako
atakuwa hana matatizo tena. Wewe nipe nafasi amini hutajuta maishani
kwa kunikubali mimi.” John aliendelea kubembeleza.
Julieth alinyamaza kimya kwa muda huku akichimba chini na kidole gumba
cha mguu wa kushoto.
“Huyu kaka tumefahamiana kwa muda mfupi sana lakini ni mtu mwenye
heshima na amekuwa karibu na mimi kwa wakati wote. Lakini zaidi ya
yote hata mimi pia nimempenda. Nikimkubali naamni hata mama
atampenda pia. Lakini je, mama atakubali niolewe katika umri huu?”
Aliwaza Julieth huku John akimwangalia kwa macho na uso wa
kumtamani.
“Nimekubali ombi lako.” Julieth hatimaye alikubali huku akiendelea
kuchimba chini na kuangalia pembeni akijaribu kuyakwepa macho ya
John.
“Nimefurahi sana Julieth nakupenda sana tutakwenda kuishi wote
Mwanza.” Aliongea John huku akimkumbatia, kumbusu na kumnyanyua
Julieth juu kama mtoto mdogo.
“Wewe! Mimi niende Mwanza nimwache mama na nani? Hapana kwanza
inabidi nikupeleke ukamwone mama umwambie lakini hilo la kwenda
Mwanza sahau.” Julieth Alimaka na Kuhamaki.
Ilikuwa ni siku ya furaha sana kwa wote na bila kupoteza muda wote
wawili walianza safari ya kwenda nyumbani kwa kina Julieth ili kuonana
na mama. Walipofika walimkuta mama Julieth akiwa amekaa sebuleni.
Julieth aliongoza kuingia ndani huku akifuatiwa na John. Julieth alimweleza
mama yake juu ya uhusiano wao na John.
Mama Julieth alichukia sana kusikia eti Julieth kapata rafiki wa kumwoa.
Kimsingi mama yake hakuwa tayari kumruhusu Julieth kuolewa katika
umri mdogo. Vilevile, mama yake Julieth alikuwa bado ana ndoto ya
kwamba Julieth atasoma hadi chuo kikuu.
“Julieth usijidanganye kabisa umri wako bado ni mdogo kuhimili
mikikimikiki ya ndoa. Lakini pia mimi bado napenda ukasome ili ndoto
yako ya kuwa daktari itimie.”Alitahadharisha mama Julieth juu ya urafiki
alionao na John.
“Hapana mama kama ni kusoma atasoma tu, na kuhusu kwamba Julieth ana umri mdogo si tatizo kwani kuna wengine wanaolewa wakiwa na umri
chini ya umri wa Julieth, lakini wanahimili vishindo vya maisha ya ndoa.”
Alifafanua zaidi John.
“Na wewe mwenyewe muolewaji unasemaji mbona umenyamaza kimya?”
Aliuliza mama Julieth.
“Mimi mama nipo tayari kuolewa naye kwani kwa kipindi cha wiki tatu
tangu nimfahamu ameonyesha moyo wa kutusaidia.” Alijibu Julieth huku
akimwangalia John kwa macho ya kusisitiza.
“Sawa! Kwa sababu yeye ameridhia hata nikimkatalia ni kazi bure. Ila nawaomba mfuate taratibu zote za kimila na kufunga ndoa rasmi ili mpate
baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwa wazazi pia.” Alishauri mama Julieth.
“Huo ni ushauri mzuri mama, lakini namwomba niende naye Mwanza nikamtambulishe kwa wazazi wangu halafu atarudi ili tufanye taratibu hizo
kama ulivyoshauri.” Aliomba John.
“Kumbe kwenu ni Mwanza?” Aliuliza Mama Julieth.
“Ndiyo mama.” Alijibu John.
“Na je maisha yenu yatakuwa wapi?” Aliuliza mama Julieth.
“Baada ya taratibu zote za kufunga ndoa kukamilika tutakwenda kuisha
Mwanza.” Alijibu John.
“Sasa baba kama mtaishi mbali na mimi nani atanihudumia, maana Julieth
ndiyo alikuwa akinisaidia. Mimi mwenyewe hali yangu si nzuri sana
naumwa mara kwa mara na Julieth anajua.” Alihoji mama Julieth.
“Hapana mama usijali mimi na mwenzangu tumekwisha jipanga namna
ya kukusaidia. Kwanza nataka uondoke hapa uhamie kwenye nyumba
nzuri nitakayokupangishia. Pia nitakuachia pesa ili uweke msichana wa
kazi ambaye atakusaidia kazi mbalimbali. Kuhusu pesa isiwe tatizo kabisa
mambo yote yatakaa sawa.” John aliongea na kuahidi kwa kujiamini huku
akimwangalia Julieth ambaye alikuwa akitabasamu muda wote wa
maongezi.
“Sawa mimi nashukuru kama mmejipanga hivyo. Mungu akubariki sana
mimi sina kipingamizi tena alimradi mmependana na kufuata taratibu za
kufunga ndoa ili mpate baraka za Mungu. Pia ninaomba mkishaanza
maisha muwe mnakuja huku kutusalimia mara kwa mara.” Mama Julieth
alishauri huku akimkazia macho Julieth na baadaye John.
“Hilo halina tatizo kabisa mama hapa ni nyumbani tutakuja bila shaka
kwani nyumbani ni nyumbani, hata hivyo kwa sasa akishawaona wazazi
wangu tu atarudi ili kukamilisha mambo ya ndoa kama ulivyoshauri.”
Alijibu John.
****************
Mikakati ya kuondoka ikaanza, mama Julieth akahamishwa kutoka
nyumba waliyokuwa wanakaa na kuhamia katika nyumba kubwa ambayo ilikuwa na kila kitu ndani. Kisha alitafutwa msichana kwa ajili ya kazi za ndani. Halafu nje ya nyumba alimfungulia duka dogo ambalo mama Julieth alikuwa akiuza bidhaa ndogondogo kama sabuni, sukari, unga na vinginevyo. Mwisho John alimnunulia mama Julieth simu kwa ajili ya mawasiliano ili kukitokea tatizo lolote atoe taarifa mapema. Mama Julieth alifurahi sana.
Siku ya kuondoka ilikaribia Julieth alionekana mwenye huzuni kwa ajili ya kumwacha mama yake. Mama Julieth yeye alikuwa katika hali ya kawaida
akisisitiza kuwa Julieth akumbuke yote aliyomwambia.

Safari ya kwenda Mwanza ilianza hatimaye walifika salama na kwenda
moja kwa moja nyumbani kwa John, maeneo ya Igoma. Julieth alishangaa sana kuona nyumba aliyokuwa akiishi John ilivyokuwa kubwa, nzuri na ya kifahari iliyojaa vitu vya thamani.
“Mpenzi nyumba yako ni nzuri sana, yaani nyumba yote hii unakaa
mwenyewe?” Aliuliza Julieth.
“Hapa ni kwako mama, nilikuwa nakaa mwenyewe na vijana wa kazi lakini sasa nina mke aitwaye Julieth naamini nyumba hii itakuwa nzuri zaidi hasa ikiwa na watoto na mke mzuri kama wewe.” John alijibu kwa kiburi na majivuno.
Julieth alitabasamu huku akizunguka huku na kule akishangaa uzuri wa
nyumba ile ya kifahari. John alipeleka mizigo chumbani na kumwelekeza kila kitu kilichomo na matumizi yake. John na Julieth waliishi maisha ya raha na furaha. John alimtembeza Julieth sehemu mbalimbali ili kumwonyesha utofauti wa mazingira ya Mwanza na Arusha. Katika kuishi kwake Arusha Julieth alikuwa hajawahi kufika Mwanza, aliupenda sana mji wa Mwanza hususan samaki aina ya sato na sangara wanaopatikana katika mji huo ambao huvuliwa katika Ziwa la Viktoria. Kwa ujumla Julieth alifurahia sana maisha yake mapya.
Baada ya wiki moja kupita Julieth alitaka kuwafahamu wazazi wa John,
lengo kuu la safari yao ilikuwa kwanza kwenda kuwafahamu wakwe zake.
“Vipi mpenzi lini tutakwenda nikawafahamu wakwe?” Aliuliza Julieth.
“Usijali mpenzi wangu tutakwenda tu kwani una wasiwasi gani, si upo na mimi kuna kazi tu zimenibana kwa sasa ila tutapanga mapema wiki ijayo.” Alimjibu John.
“Sawa John hakuna tatizo nilikuwa nataka kujua ili nimjulishe mama
Arusha.” Alijibu Julieth.
Mazungumzo yaliendelea baadaye walichoka na kwenda kupumzika.

*****Baada ya mwezi mmoja****

Wazazi wa John walikuwa wakiishi Bukoba na siyo Mwanza kama John alivyosema akiwa Arusha. Kila mara Julieth alipomwambia suala la kwenda kuwafahamu wazazi wa John aliambiwa kuwa watakwenda asiwe na wasiwasi. Baadaye kutokana na raha alizokuwa anazipata Julieth, alijisahau kabisa kama hajafunga ndoa na John. Mama yake Julieth alipokuwa
akimpigia simu na kumuuliza vipi kuhusu ndoa alimjibu hakuna tatizo mipango inaendelea vizuri. Kumbe ilikuwa ni uongo wao walikuwa wakijirusha na kusahau mambo ya ndoa na taratibu nyingine za kimila.


********Baada ya miezi mitano**************

Baada ya mapenzi na raha kushamiri, Julieth alipata ujauzito ambao hakugundua kama ana mimba. Aligundua baada ya kwenda hospitali kupima afya yake kutokana na kutojisikia vizuri ikiwa ni pamoja na kusikia kichefuchefu. Suala la mimba lilimfurahisha sana Julieth.
“Huu ndio wakati mwafaka wa kufunga ndoa, najua John atafurahi sana
nikimzalia mtoto. Akija leo nitamwambia tufanye haraka tufunge ndoa.”
Aliwaza Julieth. Ilipofika jioni aliandaa chakula cha usiku mapema huku akiwa anamsubiri
mpenzi wake arudi ampe taarifa kuhusu mimba aliyonayo. John alirudi na
kumkuta Julieth anafuraha sana.
“Kulikoni leo mpenzi mbona unaonekana una furaha sana kuna nini?” Aliuliza John.
“Mpenzi leo nimetoka hospitali kupima nina ujauzito wako na sasa
nadhani utakuwa muda mwafaka tufanye haraka tufunge ndoa.” Aliongea Julieth huku akitabasamu na kujichekeshachekesha. ”Ni vizuri Julieth lakini kwanza ukisha jifungua ndio tutafunga ndoa.” Alijibu John akionyesha kutofurahishwa na taarifa ya Julieth kuhusu
ujauzito.
“Jamani John ni muda mrefu tumekuwa pamoja kwa nini isiwe mapema kabla sijajifungua?.” Alisisitiza Julieth huku akimsogelea na kuweka mikono yake mabegani kwa John.
“Sikiliza Julieth nikwambie; ndoa ina mipango mingi sana kwa hiyo wewe nisikilize mimi.” Alisema John huku akiwa anainuka na kuelekea chumbani. John alikuwa kama mtu ambaye hajafurahia habari alizopewa na Julieth, basi Julieth alinyamaza kimya lakini aliendelea kufikiri na kutafakari hali aliyoonyesha John baada ya kupewa taarifa ya ujauzito.
“Mbona John amebadilika ghafla kuna nini? Ngoja nimwache
nitamwambia kesho vizuri.” Aliwaza Julieth huku akimfuata John chumbani.
Kesho yake asubuhi kama kawaida waliamka mapema sana, Julieth aliandaa chai. Walipokuwa wanakunywa Julieth alimwambia John kuwa angependa kwenda Arusha kuwaona mama na wadogo zake kwani ilikuwa ni muda mrefu.
“John naomba niende Arusha nikamsalimie mama na wadogo zangu.” Aliomba Julieth.
“Huko Arusha tutakwenda wote siku nitakayopanga mimi, tena nikipata muda.” Alijibu John akiwa amenuna.
“Vipi John mbona umebadilika tangu jana naona haupo sawa tukiwa tunazungumza unaonekana una hasira kuna tatizo gani?” Julieth alihoji.
“Tatizo ni wewe unaongea sana sipati hata muda wa kupumua, tena na hii chai kunywa mwenyewe.” Akaondoka na kumwacha Julieth akiwa ameduwaa.
“Huyu mwanamume amekuwaje mbona hivi jamani simuelewi.” Aliwaza Julieth. Basi Julieth akaondoa vyombo mezani na kuendelea na shughuli zake. Kadiri siku zilivyozidi kusonga mbele tabia ya John ilizidi kubadilika. Alianza kuchelewa kurudi nyumbani na akirudi anakuwa amelewa sana, tabia hizo zilimuumiza sana Julieth kwani raha alizokuwa anazipata zote
aliziona chungu na kujikuta akiwa mtu wa mawazo na kulia siku zote,
wakati mwingine alikuwa akimpiga sana na alikuwa hataki kumsikiliza kwa
chochote.
Ilifikia kipindi alimfukuza chumbani kwake akawa analala chumba cha wageni. John hakujali kama Julieth ni mjamzito alimpiga bila ya huruma, kutokana na matatizo kuwa mengi Julieth aliamua kumpigia simu rafiki yake wa kike aliyejulikana kwa jina la mama Janeth ili kuomba ushauri kutokana na matatizo aliyonayo.
Akiwa anampigia simu alikuwa chumbani bila kujua kwamba John alikuwa amejificha pembezoni mwa mlango wa kuingia chumbani akisikiliza kila kitu alichokuwa anamwambia rafiki yake. Akiwa anaendelea kuongea na simu John aliingia kwa hasira sana na kumnyan’ganya simu kisha kumpiga makofi huku akizungumza maneno makali.
“We shetani ulikuwa unazungumza na nani?” Aliuliza John kwa hasira.
“John leo unaniita shetani? Halafu unanipiga?” Aliuliza Julieth huku machozi yakimlengalenga.
“Ndio nani ulikuwa unamwambia mimi nakunyanyasa? We masikini nakuuliza mwendawazimu mkubwa na nitakuua leo na simu naichukua, hutakiwi kuwa na simu umekalia umbea tu. Nisikusikie unamwambia mtu yeyote mimi nakutesa mwehu wewe hata ukiwaambia watanifanya nini?” Wakati John akiwa anasema maneno yote hayo Julieth alikuwa akilia kwa
uchungu wa maumivu.
“Unanionea John nimekukosea nini mimi.” Alilalamika Julieth huku akishikashika na kupapasa tumbo lake.
“Nyamaza sitaki kusikia sauti yako nasikia kichefuhefu kabisa toka hapa.”
Alisema John huku Julieth akiondoka akiwa analia. Ama kweli usilolijua ni sawa na usiku wa kiza. Julieth hakujua kwa nini John amebadilika vile ghafla na kwamba nini kifanyike ili kumrudisha katika hali yake ya kawaida ilikuwa ni kitu kisichowezekana ilibidi awe mvumilivu na kujipa matumaini.
Baada ya siku kadhaa kupita hakukuwa na mabadiliko yoyote ila matatizo yalizidi kila siku ilikuwa ni ugomvi. Miezi kadhaa ilipita bila Julieth kuwa na mawasiliano na wazazi wake kwani alikuwa hana simu, hivyo ilikuwa vigumu kujua hata wazazi wake walikuwa wanaendeleaje. Kwa kweli maisha yalikuwa magumu sana. Wakati huo mimba ilikuwa na umri wa
miezi saba lakini John alikuwa hajali.
Siku moja John alimwambia Julieth kwamba siku zake za kuondoka zinahesabika. Ilikuwa ni yapata kama saa mbili usiku wakati Julieth akiandaa chakula cha jioni. John alifika na kumwita Julieth.
“We mwehu si ulikuwa unataka uende nyumbani kwenu sasa muda wako umefika unaweza ukaondoka muda wowote nakupa wiki mbili tu.” Aliongea John kwa maneno ya kutukana.
“Lakini si ulisema tutakwenda wote? Hebu niangalie na hali hii kweli ndiyo niende nyumbani mwenyewe. Afadhali nisubiri hadi nijifungue ndiyo niende nyumbani. “Wewe una kichaa nini hivi hapa ni kwako? Tena sikiliza kwa makini nataka uondoke uende popote unapopajua hata ukifa shauri yako. Kwanza hata hiyo mimba si yangu. Kwa hadhi yangu siwezi kuwa na mke kama wewe. Kwa taarifa yako mimi nina mke na mtoto na siku si nyingi anarudi sitaki aje akutane na kinyago kama wewe humu ndani.” John alitukana na kuongea kwa kebehi na dharau.
Akiwa amejiinamia Julieth alisikiliza yale maneno na kuhisi kama ni ndoto. Kabla hajazungumza lolote John aliondoka na kumwacha akiwa na mawazo sana na kushindwa kuelewa mwenziwe ana matatizo gani. Baada ya wiki moja kupita tokea John alalame na kutukana wakati Julieth akiwa amekaa sebuleni mara John aliingia na kupita pale sebuleni kama
hajamwona kisha aliingia ndani na kurudi na mabegi ya nguo na kumtupia
huku akimfukuza Julieth aondoke na kwenda kwao.
“Kuanzia muda huu ninavyoongea sitaki kukuona katika nyumba yangu
tena. Kama kuna kitu nimesahau kukitoa ukakitoe sasa hivi sitaki kukuona hapa mke wangu karibu atarudi.” Aliongea John kama mtu aliyepagawa.
“Jamani mimi nitakwenda wapi na hii mimba? John uliniambia unanipenda kweli leo unanifanyia hivi? Nakuomba kama nimekukosea unisamehe unajua hali halisi ya maisha yangu nitafanyaje mimi kama unanifukuza? Je, maisha yangu yatakuwaje? Aliuliza Julieth kwa uchungu huku machozi yakimtoka kama mtoto mdogo.
“Mbona siku uliponitoa kwetu ulionyesha kunipenda sana, halafu ukamwambia na mama….” Kabla Julieth hajamaliza kuongea machozi yalimtiririka mashavuni kama vile kamwagiwa maji kichwani.
“Mimi nikupende wewe! Mjinga sana, nimekwambia ondoka kabla sijakuua.John ”Alimfukuza Julieth na kutupa mabegi yake nje. Ilikuwa jioni yapata saa kumi na moja, Julieth alilia sana huku akiwa hajui atakwenda wapi. Aliondoka na kwenda nyumba ya jirani kidogo ambapo alikuwa anakaa rafiki yake aliyeitwa mama Janeth na kumsimulia mkasa mzima.
“Pole sana rafiki yangu wanaume wa siku hizi ndivyo walivyo, mimi nitakusaidia ulale leo, halafu kesho uende tu nyumbani kwenu Arusha. Nitakupa hela kidogo.” Mama Janeth alimwonea huruma na kumfariji.
“Asante sana mama Janeth kwani hapa nilipo sijui ningefanyaje.”
Alishukuru sana Julieth na kwenda kulala baada ya kuonyeshwa sehemu
ya kupumzika.
Usiku akiwa amelala mara akaanza kuumwa uchungu wa kujifungua,
wakati huo mimba ilikuwa na umri wa miezi saba.

Mama Janeth alimkimbiza Hospitali ya Mkoa wa Mwanza ambako alipelekwa moja kwamoja chumba cha kujifungulia. Muuguzi wa zamu alimwambia mama
Janeth aende nyumbani na awahi kuleta chai asubuhi.Julieth alijifungua salama watoto mapacha mmoja wa kike na mwinginewa kiume. Mama Janethi alipokuja asubuhi alifurahi sana kuona mgonjwawake amepata watoto mapacha bila matatizo, aliwashukuru sana wauguzi
na kuwapa shilingi elfu ishirini kama shukurani na kwa furaha aliyokuwanayo. Juliethalijifungua kabla ya miezi tisa kutokana na misukosukoaliyokumbana nayo. Hata hivyo Julieth ilibidi aendelee kukaa palehospitalini kwa muda wa miezi miwili huku akipewa huduma zote na
mama Janeth.
Baada ya miezi miwili Julieth aliruhusiwa kurudi nyumbani. Alikaa kwamama Janeth kwa muda wa mwezi mmoja akiwa anamuhudumia ili aponevizuri. Hali ya Julieth pamoja na watoto iliendelea kuwa nzuri.Siku moja wakiwa wamekaa sebuleni baada ya kula chakula cha
jioni mama Janeth na Julieth walikuwa na maongezi kuhusu John.
“Hivi Julieth, kwa nini usirudi kwa John labda akikuona na watoto
atakupokea.” Alishauri mama Janeth.
“Mama Janeth John amebadilika sana si yule wa siku zile, amekuwa mkali
kama mbogo aliyejeruhiwa. Ninaogopa sana asijeniumiza na pengine hata
kuua wanangu.” Julieth alijibu.
“Hapana jaribu kwenda na watoto kwani anajua kuwa umeshajifungua
ingawa anaona aibu ataanza vipi kuja kuwaona.” Mama Janeth aliendeleakutoa ushauri.
“Sawa! Hebu nijaribu kwenda na watoto kwani kama unavyosemaakiwaona watoto pengine atapunguza hasira.” Alijibu Julieth.Huku akiwa amewabeba watoto wake aliondoka kuelekea kwa John.Alipofika alikuwa na wasiwasi mkubwa akifikiria jinsi atakavyokabilianana uso wa John baada ya kuachana kwa takribani miezi mitatu. Alisogeajirani, akagonga taratibu na kusubiri afunguliwe. Mara mlango ulifungulwana mwanamke mwenye uso wa kujiamini kisha akaanza kumsemeshaJulieth:
“Habari za leo dada! Alisalimia.
“Salama dada yangu! Habari za hapa?” Alijibu na kuuliza Julieth.
“Karibu dada nikusaidie nini?” Aliuliza bila hata kujibu swali aliloulizwa.Julieth alishtuka sana na kuingiwa na hofu kubwa kumwona yulemwanamke aliyefungua mlango;
“Samahani namuulizia John.” Yule mwanamke alimwangalia Julieth kuanzia kichwani hadi kwenye vidole vya miguu, kisha akamkaribisha:
“Karibu ndani.” Alimkaribisha Julieth huku akitangulia ndani haraka bila hata kuangalia nyuma. Julieth aliingia na kukaa katika sofa lililokuwa jirani kabisa na mlango huku moyoni mwake akijiuliza: “Huyu mwanamke ni nani?” Wakati huo yule mwanamke alikuwa amekaa katika sofa lililokuwa karibu na mlango wa kuingia chumbani, huku mtoto wa kiume mwenye umri kati ya miaka mitano na sita hivi akichezea kijigari kidogo.
Kwa takribani dakika tatu au nne hivi walibaki kimya huku kila mmoja akimwangalia mwenzie kwa kuibia. Ghafla yule mwanamke alivunja ukimya kwa kutaka kujua Julieth alikuwa na shida gani;
“Samahani dada unamtaka John wa nini?” Aliuliza yule mwanamke. Julieth alitaka kumjibu lakini alisita. Baada ya dakika moja hivi Julieth alijipa ujasiri mkubwa na kumweleza kilichomleta pale ndani, wakati huo John alikuwa yupo chumbani asiyejua chochote juu ya nini kinachoendelea pale sebuleni:
“Mimi ni mchumba wa John, nilikuwa naishi hapa na nimetoka hospitali nimejifungua hawa watoto mapacha.” Alijieleza Julieth kwa ujasiri wa kuigiza. Yule mwanamke alishtuka na kusimama ghafla huku ameshikan kiuno na kunyoosha shingo yake kama fisi aliyesikia harufu ya mzoga.
“Wewe dada! Unajua unachoongea? Una uhakika ni nyumba hii au umekosea nyumba? Aliuliza na kuhoji yule mwanamke.
“Dada yangu sijakosea kabisa ni hapahapa.” Alijibu Julieth akiwa katika hali ya kujiamini kidogo. Yule mwanamke alimuangalia Julieth, akainama chini akitafakari jambo
kisha akaendelea kufoka;
“Hapa ni nyumbani kwangu, na huyo John unayemsema ni mume wangu.”
Huku akimnyooshea kidole yule mtoto aliyekuwa anachezea kijigari.
“Na yule pale ni mtoto wetu anaitwa Philipo. Je, huo uchumba wenu
mliufanyia mbinguni? Mbona wewe dada unanishangaza sana?” Aliendelea
kufoka.
“Kama wewe umezaa naye mtoto, mimi nimezaa naye watoto, nakuomba niitie John niongee naye.” Alifoka Julieth huku akionyesha kujiamini zaidi kuliko mwanzo.
Baada ya kuona Julieth anavyoongea kwa kujiamini yule mwanamke alisimama haraka na kuingia chumbani akimwacha Julieth na watoto wake pale sebuleni. Julieth aliinama na kuwaza kitu; “Nakumbuka siku John aliponifukuza alisema mke na mtoto wake wanakuja je, atakuwa ndio huyu? Nahisi kama naota. Lakini ni kweli yamenikuta nitafanya nini mimi?” Julieth aliendelea kuwaza na kujiuliza maswali yaliyokosa majibu.
Ni dhahiri yule mwanamke alikuwa ni mke wa John kwani alikuwa akiishi Dar es salaam akiwa masomoni katika moja ya vyuo vikuu vilivyoko huko.
John alikuwa akisafiri mara kwa mara kumtembelea na sasa alikuwa amerudi baada ya kumaliza masomo. Wakati huo wote John alikuwa anaishi na Julieth huku akimdanganya kuwa alikuwa anasafiri kikazi kumbe tayari alikuwa na mke aliyefunga naye ndoa pamoja na mtoto sasa sijui
Julieth atafanya nini. Julieth aliendelea kukaa pale sebuleni akimsubiri John. Alitumia fursa hii
kukagua sebule yote. Alitazama ukutani na kuona picha kubwa ya harusin iliyomwonyesha John akiwa na yule mwanamke aliyemkaribisha. Alishtuka na kuishiwa nguvu huku machozi yakimtoka asiamini anachokiona.
Mara mlango wa chumbani ulifunguliwa ghafla huku yakisikika maneno kama vile watu wanafokeana. John alitokeza huku yule mwanamke akimfuata kwa nyuma na kumkuta Julieth;
“Nani kakuruhusu kuja hapa kwangu wewe mbweha mkubwa?” Johnn alifoka na kutukuna bila hata salamu. Kisha akamgeukia mama Philipo;
“Hivi mama Philipo umeanza kukaribisha vichaa humu ndani?” Aliendelea kufoka John.
“Hapana mume wangu mimi huyu amekuja anakutafuta wewe kwani
unamfahamu vipi? Alihoji mama Philipo kwa upole tofauti na alivyokuwa
akiongea na Julieth.
“Huyu mwanamke ulipokuwa Dar es Salaam mke wangu, alikuwa ni mfanyakazi wangu wa ndani hapa nyumbani. Mimi nilipokuwa nasafiri alikuwa analeta wanaume hapa nyumbani taarifa nikawa nazipata. Baadaye alikuja akapata mimba na kuanza kusambaza maneno mimi ni mume wake nilimfukuza na nashangaa anataka nini tena hapa na pesa yake nilishampa
siku nyingi” Bila ya aibu na hata huruma alisema John huku akimtaka Julieth na watoto wake waondoke na asirudi tena.
“Wewe! Wewe! John! Muogope Mungu ulinichukua kwetu Arusha na kunidanganya kuwa unanipenda leo hii unaniona sifai. Eti kichaa! Baada ya kunidanganya na kuniharibia maisha yangu leo unaniona kichaa. Ungeniambia ukweli haya yote yasingetokea, kumbe ulikuwa una mke na mtoto. Sawa! mimi nitaondoka ila Mungu ndiye atakayenisaidia nakutakia
maisha mema.” Alifoka Julieth kwa mfululizo bila hata kumpa John fursa
ya kujibu huku akibubujika machozi. Wakati akizungumza maneno hayo mama Philipo alibaki kimya akitafakari kisha akaungana na John kumshambulia Julieth;
“Hebu tuondolee kilio hapa ufanye uhuni wako upate mimba halafu uje hapa na vitoto vyako nani akupokee, kamtafute baba wa watoto wako.
Unataka kunigombanisha na mume wangu toka mjinga wewe.” Alitamka mama Philipo huku akimsukumiza Julieth na watoto wake nje. Julieth alitoka akiwa analia sana. Julieth alirudi kwa mama Janeth na kumwelezea yote aliyokutana nayo.
Mama Janeth alisikitika sana na hakuwa na namna nyingine ya kumsaidia zaidi ya kumpa nauli na pesa kidogo za matumizi ili arudi kwao Arusha;
“Julieth wewe nenda tu nyumbani ukamweleze mama yako hali halisi kwani ukiendelea kuishi hapa utateseka sana na ipo siku huyo John atakutafuta. Nakutakia kila la heri Mungu atakusaidia utawalea watoto wako vizuri.” Mama Janeth alishauri.
“Nashukuru sana mama Janeth kwa msaada wako, tangu siku nilipoumwa uchungu hadi sasa. Umekuwa msaada mkubwa sana kwangu. Mimi nitakwenda nyumbani na hata huko nyumbani sijui wanaendeleaje kwani sijawasiliana nao kwa muda mrefu. Kuna siku nilimpigia mama simu ikawa haipatikani sijui wana hali gani.” Mama Janeth akampa simu ajaribu
kumpigia tena mama yake lakini haikupatikana. Julieth aliwaza moyoni
mwake;
“Jamani mama atakuwa ana matatizo gain? Labda simu itakuwa imepotea
au imeharibika.”
“Julieth unaondoka watoto hatujawapa majina, mimi ningependa huyu wa kiume aitwe Dominiki na huyu wa kike aitwe Domina au unasemaje.”
“Sawa hakuna shaka ni majina mazuri najisikia fahari nakufarijika sana kwa wewe kuwapa majina watoto wangu kwani bila wewe pengine wasingekuwepo.” Alijibu Julieth huku akiwa na mawazo mengi.
Waliendelea na mazungumzo wakala chakula cha usiku na muda wa kulala ulipofika wote walikwenda kupumzika ili kesho yake asubuhi na mapema Julieth aanze safari ya kwenda Arusha. Kesho yake asubuhi na mapema saa kumi na moja Julieth alijiandaa na kusindikizwa na mama Janeth hadi kituo cha mabasi cha Nyegezi. Basi liitwalo Jordan liliwasili, waliagana harakaharaka na safari ilianza kuelekea Arusha.
Akiwa kwenye basi alikuwa amekaa karibu na mama mmoja ambaye alimsaidia kumshika mtoto mmoja. Safari ilianza huku Julieth akiwa na mawazo mengi moyoni mwake;

“Jamani mama atakuwa ana matatizo gain? Labda simu itakuwa imepotea au imeharibika.”
“Julieth unaondoka watoto hatujawapa majina, mimi ningependa huyu wa kiume aitwe Dominiki na huyu wa kike aitwe Domina au unasemaje.”
“Sawa hakuna shaka ni majina mazuri najisikia fahari nakufarijika sana
kwa wewe kuwapa majina watoto wangu kwani bila wewe pengine
wasingekuwepo.” Alijibu Julieth huku akiwa na mawazo mengi.
Waliendelea na mazungumzo wakala chakula cha usiku na muda wa kulala ulipofika wote walikwenda kupumzika ili kesho yake asubuhi na mapema Julieth aanze safari ya kwenda Arusha.
Kesho yake asubuhi na mapema saa kumi na moja Julieth alijiandaa na
kusindikizwa na mama Janeth hadi kituo cha mabasi cha Nyegezi. Basi liitwalo Jordan liliwasili, waliagana harakaharaka na safari ilianza kuelekea Arusha.
Akiwa kwenye basi alikuwa amekaa karibu na mama mmoja ambaye alimsaidia kumshika mtoto mmoja. Safari ilianza huku Julieth akiwa na
mawazo mengi moyoni mwake;
“Nikifika sijui nitaanzaje kumweleza mama. Kwa matatizo yake ya moyo (shinikizo la damu) sijui atalipokeaje swala hili.” Aliendelea kuwaza huku gari likichanja mbuga.
Safari iliendelea hatimaye walifika Arusha saa kumi na mbili za jioni.
Julieth alipoteremka tu alianza kuangalia huku na kule akishangaa
mabadiliko ya mji ule kama mgeni. Alichukua teksi na kwenda moja kwa moja nyumbani kwao mtaa wa Kaloleni katika nyumba aliyomwacha mama yake. Wakati anamlipa dereva teksi, mara dada mmoja aliyetokea nyuma yake akamwita kwa mshangao;
“He! Julieth! Julieth! Umerudi Julieth!” Akamkumbatia yeye na watoto
wake pamoja.
“Jamani za siku nyingi.” Aliendelea kumsemesha Julieth. Mwanzo Julieth hakumtambua lakini alivyozidi kumwangalia akamkumbuka.
“Oh! Kumbe Zubeda! Mambo vipi rafiki yangu? Nimefurahi sana
kukuona habari za hapa?” Zubeda alikuwa ni rafiki yake Julieth, kwani walikuwa wakiuza chapati pamoja wakati Julieth akiwa Arusha.
Domina alianza kulia, haraka Zubeda alimchukua Dominiki ili Julieth
amnyonyeshe Domina.
“Habari za hapa ni nzuri kiasi.” Aliongea Zubeda huku akimshika vizuri
mtoto.
“Nzuri kiasi!” Alihamaki Julieth huku akimkazia macho Zubeda.
“Ndiyo! Nzuri kidogo.” Alisisitiza Zubeda huku akiyakwepa macho ya
Julieth.
“Vipi mwenzangu mbona ulikuwa kimya sana? Wakati mama yako akiwa anaumwa tulikupigia simu mara nyingi lakini haikupatikana na …”
“Ehe! Sasa anaendeleaje?” Julieth alimkatisha Zubeda na kuuliza akiwa
katika hali ya kushtuka.
Zubeda aliwachukua watoto wa Julieth na kukaa nao pembeni wakati yuleN dereva akiondoka. Julieth alitaka kuingia ndani moja kwa moja lakini Zubeda alimzuia.
“Julieth wadogo zako na mama yako hawapo hapa.” Zubeda alianza
kueleza. Kama nilivyokudokeza mama yako aliugua sana, tulikutafuta kwenye simu yako ili utume fedha za matibabu bila mafanikio. Kwa vile mama yako alikuwa hana pesa ikabidi auze simu yake ili apate pesa za matibabu.”
“Oh! Samahani sana. Simu yangu iliharibika nikawa na simu nyingine.
Lakini namba ya mama ninayo, ila nilishawahi kumpigia lakini
haikupatikana. Labda ndo kipindi alipoiuza. Aliongea Julieth kwa
masikitiko.”
“Lakini mbona hata mume wako tulimpigia simu hakupokea, tuliamua
kumtumia ujumbe lakini hakujibu. Hivi kwa nini mlikuwa mnafanya hivi?”
Aliendelea kuhoji Zubeda huku Julieth akimsikiliza kwa makini sana.
“Ni histora ndefu hebu nitulie kwanza nitakusimulia siku nyingine wewe
ni rafiki yangu sitakuficha kitu. Eh! Hebu niambie mama na wadogo zangu wanaishi wapi sasa?” Julieth alihoji zaidi.
“Wadogo zako waliondoka kutokana na kushindwa kulipa kodi ya
nyumba, kwa sasa sijui watakuwa wapi.” Alijibu Zubeda.
“Eh! Na mama?. Aliuliza Julieth.
Zubeda alimwangalia usoni Julieth ambaye alikuwa akionyesha uso wenye maswali mengi sana. Kwa muda wa dakika moja hivi Zubeda aliwaza na kutaka kumdanganya Julieth kuhusu aliko mama yake. Lakini mwisho aliamua kumwambia ukweli.
“Baada ya kuugua kwa muda mrefu mama yako ali…” Alisita kidogo
Zubeda.
“Alifanya nini?.” Julieth aliuliza.
“Alifariki dunia.” Zubeda alijibu huku akimpa pole Julieth.
Julieth aliyekuwa amesimama alipiga kelele na kuanguka chini puu! Huku nguvu zikimwishia. Alilia sana kama mtoto aliyeungua moto.
“Mamaaa! Mamaaa! Mama yangu wee! Upo wapi mama! Siamini nipeleke nikamwone. Nipeleke! Nipeleke!” Aliendelea kulia, kugagaa chini na kutamka maneno mbalimbali kwa uchungu sana. Hata hivyo haikusaidia kitu mama yake alikuwa ameshafariki na kuzikwa siku nyingi sana. Julieth alikuwa ameishiwa nguvu kabisa hivyo Zubeda aliwabeba watoto wote. Ilikuwa yapata kama saa mbili hivi za usiku, Julieth alinyanyuka kwa nguvu za ajabu na kugonga geti la nyumba aliyokuwa akiishi mama yake huku akiita ;
“Mama fungua mimi mtoto wako Julieth nimerudi.”
“Hapo kuna mpangaji mwingine Julieth unawasumbua watu bure.”
Zubeda alimkataza Julieth. Lakini Julieth hakutaka kumsikiliza. Kutokana na geti kugongwa kwa nguvu alitoka kaka mmoja na kufungua.
“Vipi dada una matatizo gani?” Aliuliza yule kaka.
“Yuko wapi mama yangu, namtaka mama yangu.” Aliuliza Julieth huku
akilia na akiwa katika hali ya kuchanganyikiwa.
Yule kaka hakumwelewa anachozungumza akabaki anamshangaa. Ghafla Julieth alianguka chini na kuzimia. Yule kaka na Zubeda walisaidiana kumnyanyua Julieth na kumwingiza ndani kisha wakamlaza chini huku feni ikimpepea. Yule kaka akamuuliza Zubeda aliyekuwa amewabeba watoto wa Julieth.
“Vipi huyu mwenzio ana matatizo gani?” Aliuliza yule kaka.
Zubeda akamwelezea kila kitu yule kaka ambaye ndiye mpangaji mpya
katika ile nyumba, alimwonea huruma sana Julieth. Baada ya Julieth
kuzinduka aliendelea kulia asijue nini cha kufanya kwa yote yaliyomkuta.
“Usijali Julieth nitakusaidia ulale hapa mpaka kesho. Karibu sana mimi
naitwa Baraka, Zubeda amenieleza matatizo yote uliyonayo pole sana.”
Aliongea Baraka ili kumfariji Julieth.
“Asante sana kaka Baraka.” Alishukuru Julieth.
Baraka alimtayarishia maji ya kuoga na baada ya kuoga Julieth alijisikia
vizuri sana kisha alipewa chakula. Muda wa kulala ulipofika Baraka
alimwonyesha Julieth chumba cha kulala akiwa na watoto wake Domina
na Dominiki. Alipokuwa chumbani aliwaza mambo mengi sana huku moyoni akijilaumu mwenyewe;
“Mimi ndio chanzo cha kila kitu, hivi kwa nini niliondoka na kumuacha
mama yangu wakati nilijua anaumwa?, Ewe mama popote ulipo naomba
unisamehe na wadogo zangu Joseph na Peter sijui wako wapi, maisha
yangu ni ya mateso siku zote kwa nini lakini? Sijui nitakwenda wapi. John alinidanganya na kuniacha, sasa na mama nimempoteza mimi nitakuwa mgeni wa nani?” Alilia kwa uchungu huku akiwaangalia watoto wake waliokuwa wadogo sana wasioelewa chochote, baadaye akalala usingizi mzito kutokana na uchovu wa mawazo na safari.
Kesho yake asubuhi Baraka aliamka mapema na kuandaa chai mezani
kisha akamwamsha Julieth ajiandae wakapate kifungua kinywa. Wakiwa
mezani Baraka alitaka kumfahamu vizuri Julieth. Maskini Julieth
alimweleza kila kitu kuhusu mkasa mzima wa maisha yake na pia
akamwambia hajui atakwenda wapi.Yule kaka akamwambia ataendelea
kuishi pale ili aweze kuwalea watoto wake vizuri na pia atamsaidia
kuwatafuta wadogo zake. Julieth alimshukuru sana Baraka kwa kumpa
nafasi ya kuishi pale nyumbani kwake. Baraka alikuwa ni mfanyabiashara palepale mkoani Arusha. Alimsaidia sana Julieth na kumfariji wakati wote kwani Julieth alikuwa amekata tamaa ya maisha.
Baada ya siku kadhaa kupita Julieth alianza kuzoea mazingira, aliishi vizuri na watoto wake. Baada ya mwaka mmoja Julieth na Baraka walianza uhusiano wa kimapenzi. Urafiki wao ulimfanya Julieth asahau yote aliyotendewa na John. Maisha yaliendelea na hatimaye Julieth na Baraka wakawa wapenzi na baadaye walifunga ndoa kanisani. Wazazi wa Baraka walimpenda sana Julieth na kuwatakia kila la heri katika maisha yao. Baraka aliwapenda sana watoto wa Julieth na hatimaye hata jina la ukoo walitumia jina la Baraka.
Julieth hakutaka kumkumbuka John kabisa na wala hakutaka kumsikia
tena katika maisha yake. Wakati huo Julieth alikwisha wapata wadogo zake na kuishi nao kwa furaha sana kama familia moja. Watoto wa Julieth walikua wakimjua baba yao ni Baraka.

**********Baada ya miaka mitatu************

Baada ya miaka mitatu Julieth alifanikiwa kumpata mtoto mwingine wa
kiume aliyeitwa Novatus. Julieth alifurahi kuliko kawaida kwani familia
ilizidi kuongezeka. Maisha yao yalikuwa mazuri sana kuliko yalivyokuwa kwa John. Kwani kwa Baraka waliishi kwa amani na upendo.
Huko Mwanza katika maisha ya John yalibadilika, biashara zilimwendea
vibaya na kuanza kuuza baadhi ya vitu. Siku moja wakiwa wanatoka
kwenda katika matembezi John na mke wake pamoja na mtoto wao
wakiwa katika gari . walipata ajali mbaya sana. Mke wake pamoja na mtoto walifariki dunia palepale ila John alipoteza fahamu na kuumia baadhi ya sehemu katika mwili wake. John alikimbizwa hospitali ambako alikaa muda mrefu sana akiwa anatibiwa. Kutokana na kushindwa kunyanyuka kitandani alishindwa kuhudhuria hata mazishi ya mtoto na mke wake, hata hivyo baadaye alipona na kuruhusiwa.
Lakini wakati akiondoka, daktari alimwambia kuwa kutokana na ajali
aliyoipata hata kuwa na uwezo wa kuzaa tena. Ilikuwa ni mshtuko sana
kwa John ambaye alikuwa hana mtoto mwingine tena zaidi ya Philipo
aliyefariki kwenye ajali. John alichanganyikiwa.
Baada ya kupata nafuu John aliruhusiwa kurudi nyumbani. Siku ya tatu
tangu atoke hospitali, John alikuwa amekaa chini ya mti wenye kivuli
kikubwa alianza kuwaza juu ya mambo yaliyokuwa yanaendelea kutokea dhidi yake.
“Kweli mimi yamenikuta, sina mke, sina mtoto halafu sina uwezo wa
kupata mtoto maisha yangu yote. Maisha yangu yamefika mwisho na
biashara nazo zinaniendea vibaya nitafanyaje?”
Akiwa anawaza ghafla akamkumbuka Julieth ambaye alizaa naye watoto
mapacha kisha akamfukuza baada ya mke wake kurudi kutoka Dar es
Salaam; “Julieth ana watoto wangu mapacha sijui atakuwa wapi, labda
atakuwa kwao Arusha na kwa mabaya yote niliyomfanyia na sasa ni miaka mitano imepita itanibidi nimtafute alipo ikibidi niende Arusha.” Aliwaza John huku akiwa na matumaini atakapomuona Julieth atawapata watoto wake. John alianza kuulizia wapi Julieth alipo baadaye aligundua Julieth yupo Arusha na moja kwa moja alipanga safari ya kwenda kumtafuta Julieth.
Baada ya wiki moja John alianza safari ya kwenda Arusha kumtafuta
Julieth. Akiwa njiani aliwaza sana moyoni;
“Nikimpata nitamwomba msamaha kwa yote niliyomfanyia halafu tuanze maisha mapya na watoto wetu.” Aliwaza John huku safari ikiendelea.
Alipofika Arusha alichukua teksi kuelekea nyumbani kwa akina Julieth.
Kutokana na kwamba nyumba ile anaikumbuka kwa hiyo alikwenda moja kwa moja. Ilikuwa yapata saa moja jioni ambapo Julieth pamoja na familia yake walikuwa wamekaa sebuleni wakizungumza huku geti likiwa wazi. John alipofika alipita moja kwa moja na kwenda kugonga mlango wa sebuleni. Mlango ulifungualiwa na mdogo wake Julieth yaani Joseph ambaye alimkaribisha ingawa alikwisha msahau kutokana na mabadiliko aliyokuwa nayo baada ya kupata ajali. Ilikuwa ni miaka mingi imepita tangu waonane, kwa mshtuko mkubwa sana Julieth aliyemtambua alinyanyuka na kusema.
“Nani amekuruhusu uingie humu ndani? Hivi wewe ni binadamu wa aina gani umeona haitoshi uliyonifanyia bado unanifuatafuata, unataka kuniua au? Naomba utoke nje sasa hivi.” Alisema Julieth huku midomo
ikimtetemeka kwa hasira na kuwaacha waliokaa pale sebuleni wakishangaa kuna nini.
“Vipi mke wangu huyu mtu ni nani?” Aliuliza Baraka.
“Huyu ndiye John aliyenitesa katika maisha yangu, nashangaa amefuata
nini hapa.” Alijibu Julieth.
John aliyekuwa amesimama alianguka chini kwa magoti na kuanza kulia huku akiomba msamaha;
“Julieth naomba unisamehe najua nimekukosea sana katika maisha yako
na mimi Mungu amenipa pigo la maisha hapa nilipo sina uwezo wa kuzaa tena. Nilipata ajali mke na mtoto wangu walifariki, naishi katika mazingira magumu. Julieth naomba unisamehe unipe nafasi ya kuwa karibu na watoto wangu nakuomba Julieth.” Alibembeleza John.
“Kweli malipo ni hapahapa leo hii wewe unanipigia mimi magoti, baada
ya kunifukuza kama mbwa na kuwakana watoto leo unasema unataka uwe karibu na nani?. Una kichaa kweli wewe, hawa watoto sio wako yule pale ndio baba yao anaitwa Baraka. Mimi sikujui na wala sitaki kukuona naomba uondoke” Alifoka Julieth huku akicheka kicheko cha kejeli.
“Kama ni kukusamehe nilikwisha kusamehe ila naomba uondoke na
watoto wangu uwasahau.” Alisisitiza Julieth huku akisimama na kuelekea chumbani akibamiza mlango kwa hasira.
John hakuwa na cha kusema zaidi, aliwaangalia Domina na Dominiki
watoto ambao walikuwa hawaelewi chochote. Watoto nao walimshangaa sana John wakimwacha na maumivu zaidi moyoni akilia kwa uchungu. Aliaga na kuondoka huku akitembea hatua moja na kugeuka nyuma kuwaangalia watoto wake ambao hakuwa na uwezo wa kuwachukua tena. Julieth na mume wake walibaki wakiwa wanatafakari kilichotokea, Julieth alikuwa ni mtu mwenye hasira sana siku hiyo.
John aliondoka akiwa amechanganyikiwa asijue anaelekea wapi. Ghafla
akiwa anavuka barabara aligongwa na gari na kufa palepale ukawa mwisho wa maisha yake.
Julieth na watoto wake walibaki wakiwa katika maisha ya furaha na amani na kwa Julieth Baraka ndiye alikuwa chaguo lake la moyo walipendana sana wakaishi maisha ya furaha na amani.

MWISHO

Post a Comment

0 Comments